Jumapili, 31 Mei 2015

WAZAZI KAMPALA UNIVERSITY(KIU) KUANDAMANA



WAZAZI na walezi wa wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi katika chuo cha kimataifa cha Kampala(KIU), wamepanga kuandamana kwenda chuoni hapo ili kupata ufafanuzi kuhusu madai ya watoto wao kuhusu usajili kamili wa kozi ya famasia.
Wakizungumza kwa wakati tofauti na MTANZANIA wazazi hao wamesema wameamua kujikusanya ili watambuane na kujua hatima ya watoto wao kielimu.
Mmoja wa wazazi hao aliyejitambulisha kwa jina la Hassan Bumbuli alisema wametengeneza kundi kwenye mitandao ya simu inayowawezesha kuwasiliana ili kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo.
“Sisi ndio tunalipa ada na ndio tunaojua ada tunapata wapi, Chuo itabidi kitueleze ukweli ni lini watasajili kozi na si kutudanganya kama wanavyowaambia wanafunzi kwani sisi si watoto wadogo,” alisema Bumbuli.
Alisema ilibidi wawaambie watoto wao waahirishe muhula mpaka hapo kozi hizo zitakaposajiliwa lakini uongozi wa Chuo hicho unawakatalia kitu ambacho kinawatia hofu.
Naye Mohamed Khasimu alisema chuo kimekuwa na gharama zisizojulikana kama kulipia mitihani na gharama nyingine ambazo kipindi cha mkataba hazikuwepo hivyo wataenda chuoni hapo kabla ya mitihani kuanza ili kupata maelezo ya kina.
“Tutakutana na Uongozi wa Chuo watujibu madai ya watoto wetu kama hatutoridhika basi tutajua nini cha kufanya,” alisema Khasimu.
Alisema wototo wao wamekuwa wakikaripiwa na kutishiwa kufukuzwa chuo kila walipojaribu kuhoji usajili wa kozi.
Hivi karibuni wanafunzi wa kada ya famasia chuoni hapo waligoma kuingia darasani kuushinikiza uongozi kutoa ufafanuzi kuhusu usajili wa kozi wanazosoma pamoja na madai mengine sita.
                                                   


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni