Jumatatu, 18 Mei 2015

DIWANI KISARAWE II AWAONYA WANACCM




DIWANI wa kata ya Kisarawe II, Manispaa ya Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam, Issa Zahor amewataka wanachama wa Chama cha Mapinduzi  kuvunja makundi ndani ya chama hicho pindi tu kura ya maoni inapomalizika.
Akizungumza na MWANDISHI wa blog hii jana jijini hapa, Zahor alisema makundi ya kura za maoni yanatakiwa kuvunjwa kabla ya kuingia katika uchaguzi mkuu.
Alisema wanachama wa chama hicho wanapaswa kumuunga mkono mgombea aliyepita na si kuhamia upinzani.
“Mara nyingi makundi yamekuwa hayavunjwi kiasi ambacho yanakigharimu chama katika chaguzi mbalimbali kwa upande mmoja kuunga mkono upinzani,” alisema Zahor.
Alisema amelazimika kusema hayo kutokana na matokeo ya uchaguzi wa serikali za mitaa kuwashitua ambapo katika mitaa 11 ya kata hiyo, saba walichukua wapinzani na mitano kuchukuliwa na CCM.
“Matokeo ya upinzani kuchukua viti vingi vya mtaa kumetokana na kutokuwa na umoja ndani ya CCM,” alisema.
Akizungumzia kuhusu Ilani ya CCM, Zahor alisema ametekeleza kwa asilimia kubwa kwani amesimamia uchimbaji wa visima kwa kila mtaa.
“Tumetekeleza ilani ya CCM kwani mpaka sasa kuna kisima cha maji kila mtaa na kuwapunguzia muda mrefu waliokuwa wakitumia kinamama kutafuta maji ,” alisema.
Alisema kwa upande wa miundombinu pia wamefanikiwa kutengeneza barabara zinazoingia na kutoka katani hapo pamoja na zile za mitaani.
Aliwataka wananchi kuendelea kumuunga mkono katika uchaguzi ujao ili akamilishe na kuendeleza mambo ambayo bado hayajakamilisha pamoja na kutekeleza Ilani

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni