Wednesday, August 9, 2017

atakayefanya udanganyifu vyei vya kuzaliwa na vifo kukiona



WAKALA wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) kwa kushirikiana na Bodi ya mikopo ya elimu ya juu(HESLB)wametoa onyo kali kwa wanafunzi wa vyuo vikuu watakaofanya udanganyifu wa vyeti vya kuzaliwa na vifo ili wapatiwe mkopo.
Onyo hilo limetolewa leo jijini Dar es Salaam na Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa wa RITA, Emmy Hudson alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Alisema wametoa onyo hilo kutokana na kubainika kwa vyeti kughushi takribani 500 vya kuzaliwa na vifo kwa waombaji wa mikopo ya elimu ya juu kwa mwaka wa masomo 2016/17.
Alisema vyeti hivyo havikuwa katika kumbukumbu zao na hivyo walishindwa kuvitambua.
“Sheria ya vizazi na vifo inamtia hatiani mtu yeyote ambaye atatoa taarifa za uongo hivyo vyombo vya dola vitawashughulikia wanaofanya udanganyifu huu,” alisema Emmy.
Alisema kwa kushirikiana na HESLB wameanzisha mfumo maalumu wa uhakiki kwa kutumia mtandao ambapo mwombaji atatuma cheti cha kuzaliwa na vya vifo kutumia email na vitahakikiwa.
“Waombaji watatakiwa kuhakikiwa katika ofisi za wilaya zilizotoa vyeti hivyo na makao makuu ya RITA na walioko mbali watumie barua pepe ya uhakiki@rita.go.tz wakiambatanisha vyeti na risiti za benki baada ya kulipia,” alisema Emmy.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Abdulrazaq Badru alisema wanufaika wa mikopo wanatakiwa kuwasilisha cheti cha kuzaliwa , vyeti vya masomo na vyeti vya vifo kama alifiwa na wazazi wake.
“Nyaraka hizi ni muhimu sana katika usajili wa wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu ili kupata wanaostahili kunufaika,”alisema Badru.
mwisho