RAIS Jakaya Kikwete ameitaka Manispaa ya
Kinondoni kubomoa nyumba zote zilizojengwa kwenye mikondo ya kupitisha maji
huku akiwataka wakazi wa mabondeni kuhama mara moja.
Akizungumza na wakazi wa Manispaa ya hiyo mara
baada ya kukagua athari za mafuriko zilizotokea baada ya kunyesha kwa mvua,
Rais Kikwete alisema kuwa, athari ya mvua ni kubwa kuliko watu wanavyofikiria.
Alisema, nyumba ambazo zimejengwa kwenye mikondo
ya kupitisha maji zinapaswa kubomolewa ili kuruhusu yaweze kuelekea baharini,
jambo ambalo linaweza kupunguza kutokea kwa mafuriko.
Alisema Manispaa inapaswa kuchukua hatua za
dharura za kutatua matatizo hayo ikiwa ni pamoja na kujenga mitaro inayoweza kupitisha
maji kwa haraka ili kuondoa tatizo hilo.
“Ninawaagiza watendaji kubomoa nyumba
zilizojengwa kwenye mikondo inayosafirisha maji ambayo imechangia kuongezeka
kwa mafuriko katika maeneo mbalimbali.
“Mpango kama huo ulifanywa na wakazi wa Buruguni
ambapo Manispaa ya Ilala ilibomoa nyumba 17 zilizojengwa kwenye maeneo ya kupitisha maji , jambo ambalo lilichangia
kupunguza ukubwa wa tatizo,”alisema Kikwete.
Alisema, tangu watatue tatizo hilo,hakuna nyumba
iliyoingiliwa na maji katika mvua
zinazoendelea kunyesha.
Aliwashangaa mpaka sasa watendaji wa Manispaa
hiyo wameshindwa kutumia maarifa ya kuondoa maji kwenye makazi ya watu hadi
yamesababisha malalamiko.
“Ninashangaa
mpaka leo hamjafanya lolote huku wananchi wakikimbia nyumba zao, jambo ambalo
limeongeza malalamiko, kutokana na hali hiyo, mnapaswa kutumia maarifa ili kutatua
kero hii,”alisema.
Aliongeza, Manispaa Kinondoni ina bahati kwa
sababu Mkurugenzi wake ni Mhandisi, lakini ameshindwa kutumia maarifa ya
kuondoa maji kwenye nyumba za watu mpaka wananchi wamekimbia nyumba zao.
“Wewe si
Mhandisi? taaluma yako unaitumiaje! Umeshindwa hata kutafakari kidogo namna ya
kutatua tatizo hili mpaka leo, haya nimewaletea maarifa yangu ingawa ni ya
kizee lakini yatawasaidia kutatua tatizo,”alisema.
Alibainisha, Manispaa hiyo imepenga kutekeleza
mpango wa muda mrefu ambao una gharama kubwa ya
utekelezaji wake bila ya kutafakari mpango wa dharura wa kutatua tatizo
lililopo.
“Mmekuja na gharama kubwa za utekelezaji wa
mpango wa muda mrefu wa kutengeneza mitaro huku mkishindwa kutafakari mpango wa
dharura wa kuondoa maji kwenye makazi ya watu, hilo ni tatizo,”alisema Kikwete.
Alisema Manispaa ina pampu 28 ambazo zinafanya
kazi mpaka sasa lakini wameshindwa kuzipeleka kwenye maeneo hatarishi ambayo
yaliyoathirika zaidi na tatizo hilo, badala yake wamesambaza moja moja mtaani
huku maji yakishindwa kuondoka.
“Kitendo cha kusambaza pampu moja moja kwenye
makazi ya watu hakujasaidia lolote, hata kama mlitaka kuwafurahisha watu lakini
hawawezi kuwashukuru, hivyo basi mlipaswa kuzichukua zote mkazipeleka sehemu
moja ili ziweze kunyonya kwa maji kwa haraka na kuhamishia sehemu
nyingine,”alibainisha.
Akizungumza mara baada ya kukagua ofisi za Ofisi
za Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka
Dar es Salaam (Dawasa) eneo la Tegeta ambazo zimezingilwa na maji, Rais Kikwete
alisem akuwa mamlaka hiyo inapaswa kukaa na Wakala wa Barabara(TANROADS) na
Manispaa ya Kinondoni ili kuangalia namna ya kuondoa maji yaliyojaa kwenye
ofisi hizo.
Alisema ili maji yaweze kuondoka kwenye maeneoe hayo, lazima wajenge
mifereji ya kupitisha maji ambayo yataelekea baharini moja kwa moja bila ya
kuathiri makazi ya watu.
Hata hivyo, Kikwete aliwataka wakazi wote wa mabondeni na maeneo
hatarishi kuhama sehemu hizo na kwenda kujiandikisha kwenye ofisi za Manispaa
ili waweze kupewa viwanja.
Alisema maeneo ambayo tayari washalipwa hawezi kulipwa tena ila wale
ambao hawajapewa maeneo na wako tayari kuhama serikali itawapa viwanja.
“ Kuna baadhi ya watu washalipwa lakini mpaka sasa bado wanaendelea
kung’angania maeneo haya ambayo ni hatarishi kwa maisha, hakuna jawabu zaidi ya
kuondoka tu, kwa sababu serikali haina uwezo wa kuzuia mvua,”alibainisha
Kikwete.
Hata hivyo, Mkurugenzi wa Manipaa
hiyo, Mhandisi Mussa Naty alisema kuwa Manispaa hiyo imepanga kutumia Sh
bilioni 3.5 kwa ajili ya kujenga mitaro katika maeneo mbalimbali ya manispaa.
Alisema kiasi hicho ni kikubwa hivyo basi hawana uwezo wa kuzipata
katika kipindi hiki zaidi ya kuiomba serikali kuu iwasaidie.
“Tutatumia pampu zetu kuondoa maji kwenye maeneo hatarishi ili wananchi
waweze kurudi kwenye makazi yao, lakini pia kuna wengine ambao wamejenga kwenye
maeneo ya kupitisha maji ambayo yamesababisha athari hii kuongezeka,’alisema
Naty.
Alisema wakati wanajaribu kutatua tatizo la maji kutuhama katika eneo
la Dawasa walimtafuta mkandarasi kutoka China ili aweze kutengeneza mitaro ya
maji lakini walikwama baada ya kutaja gharama kubwa.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni