Jumamosi, 16 Mei 2015

MVUA ZAKWAMISHA MAKABIDHIANO YA DARAJA




MVUA zawa sababu za kusogezwa mbele kwa makabidhiano ya Mradi  wa ujenzi wa daraja la kisasa la Kigamboni ambao mpaka hivi sasa umekamilika kwa asilimia 80.
Meneja wa mradi huo kutoka NSSF, Karim Mataka, aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kuwa wanatarajia ifikapo Desemba watakuwa wamekamilisha ujenzi lakini mwishoni mwa mwezi Septemba au mwanzoni mwa Oktoba daraja linaweza kuanza kutumika na watembea kwa miguu.
Alisema changamoto mbalimbali zimechangia kwa asilimia kubwa kuchelewa kukamilika kwa daraja hilo ambalo awali lilikuwa likamilike Januari 31 lakini kutokana na baadhi ya changamoto zilizojitokeza ikasogezwa hadi mwezi Julai na sasa wanatarajia kuukamilisha mwishoni mwa mwaka huu.
Alisema mpaka sasa mradi huo umeshaghalimu bilioni 240 na kwamba baada ya kukamilika ndio watataja gharama halisi iliyotumika katika ujenzi wa daraja hilo.
Aliongeza kuwa serikali imeiruhusu NSSF kumalizia ujenzi wa barabara ya mapokeo kwa kiwango cha lami yenye urefu wa kilomita 2 ile Vijibweni kwenda kwenye maungio ya barabara ya Kibada.
“Pamoja na changamoto zilizotufanya kuchelewa kidogo lakini tunashukuru tunaenda vizuri na daraja letu litakuwa na barabara sita ambazo tatu zitakuwa zikitokea Kigamboni na tatu zitakuwa zikielekea Kigamboni,” alisema Mataka.
Alisema ujenzi wa daraja hilo linasimamiwa na wahandisi kutokana TANROADS, Wizara ya Ujenzi pamoja na NSSF.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni