Jumamosi, 9 Mei 2015

CCM wilaya Morogoro acheni ukandamizaji



WAJENZI wa vibanda vya biashara vinavyotengeneza uzio wa uwanja wa maonyesho wa sabasaba Morogoro, wamelalamikia kunyanyaswa na Ally Issa, Katibu wa wilaya wa Chama cha Mapinduzi(CCM) mkoani humo.
Akizungumza kwa niaba ya wenzake mmoja wa wajenzi hao, Robert Mluge alisema mwaka 1989 walijenga vibanda  kuzunguka uwanja huo kwa makubaliano na manispaa ya morogoro kuwa wao ndio watakuwa wamiliki wa vibanda huku manispaa ikimiliki sehemu ya uwanja.
 Alisema lengo lilikuwa ni kuweka uzio wa uwanja wa maonyesho wa  sabasaba ambapo mjenzi alijenga kwa kuelekeza milango nje ili afanye biashara zake huku manispaa ikiendelea na maonyesho ya sabasaba kwa ndani.
“Manispaa ilitutafuta yenyewe kwa kutushawishi kupitia Afisa Utamaduni wa manispaa ya Morogoro aliyejulikana kwa jina moja la Ntemo. Tulikubali kujenga kwa makubaliano sisi kumiliki vibanda na wao kumiliki uwanja,” alisema Mluge.
Alisema mnamo 2007 Chama cha Mapinduzi wilaya ya Morogoro waliwataka wajenzi hao kulipa kodi ya pango ya shilingi 150,000 kwa kila kibanda kwa madai kuwa wao ndio wamiliki halali wa uwanja huo.
Alisema baada ya wao kukataa kuilipa CCM fedha hizo walivunjiwa vibanda vyao na kunyang’anywa mali na vitu vyao kama mashine na majokofu na kuuzwa kwa mnada  na dalali aliyejitambulisha kutumwa na CCM, G. Mwambogela kutoka Majembe Auction Mart.
Alisema CCM iliwashitaki wajenzi hao mara kadhaa katika mahakama na mabaraza ya ardhi na hukumu zilionyesha kuwa wajenzi wanahaki hivyo kukitaka chama hicho cha siasa kuwarudishia vibanda na kuwalipa mali zao walizoziuza.
Kwa mujibu wa hukumu iliyotolewa na msajiri wa mahakama kuu kitengo cha ardhi L, M Mlacha, imeeleza kuwa maombi yaliyotumwa na CCM kwa ajili ya utekelezaji wa kuwafukuza na kufungua milango madai hayo hayana msingi wa kisheria, ni potofu na awalipe gharama.

Baada ya hukumu hiyo Wajenzi walimuandikia Katibu Mkuu wa CCM kumtaka amuamuru Katibu wa wilaya wa chama hicho lakini mpaka sasa hawajajibiwa.






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni