Jumapili, 31 Mei 2015

MBARONI KWA KUJIFANYA ASKARI WA JIJI




MKAZI wa Kariakoo Mjini Dar es Salaam Godfrey Kwikwilukiza (33),jana amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Mwanzo Kariakoo akikabiliwa na tuhuma za kujipatia kiasi cha fedha Sh 20,000 kwa njia ya udanganyifu.
Akisomewa shtaka hilo mbele ya Hakimu Mkazi Christine Ruguru,Karani wa Mahakama hiyo Lucy Rutabanzibwa, alidai kuwa mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo Mei 23 mwaka huu eneo la Stesheni.
Rutabazibwa alidai Mahakamani hapo kwamba mtuhumiwa alijipatia fedha hizo toka wa mtu mmoja anayejulikana kwa jina la Shabaan Salum, kwa kudanganya kuwa yeye ni askari wa jiji.
Mshtakiwa alikana kutenda kosa hilo na upelelezi wa shauri hilo bado unaendelea ambapo Hakimu alidai kuwa mshtakiwa anatakiwa alete wadhamini wawili wenye barua kutoka serikiali za mitaa watakaoweka bondi ya maandishi ya Sh. Laki 1 kwa kila mmoja.
Hata hivyo mshtakiwa alirudishwa mahabusu kwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana hivyo kesi hiyo itakuja tena kusikilizwa hoja za awali Juni 11 mwaka huu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni