MLEZI wa asasi ya kiraia inayohudumia wasichana wanaotoka
katika mazingira magumu (New Hope for Girls organization), Consoler Wilbert,
amewaomba wananchi kumchangia nauli ya kwenda kwenye matibabu nchini India
baada ya hospitali hapa nchini kumpa rufaa akatibiwe huko.
Consoler ambaye amekuwa ni muhanga wa unyanyasaji wa watoto
wa kike, alisema anasumbuliwa na maumivu ya kichwa na mgongo mara kwa mara yaliyotokana
na kupigwa kwa masaa sita na walimu wake wakati akisoma sekondari ya Jitegemee
iliyopo jijini Dar es Salaam.
Akizungumza kwenye uzinduzi wa maadhimisho ya siku ya hedhi
salama duniani jijini Dar es Salaam Consoler alisema alilazimishwa kuolewa
akiwa na umri mdogo na alipokataa alikuwa anapigwa mara kwa mara shuleni na
nyumbani.
“Siku moja nilipigwa sehemu mbali mbali za mwili hasa
kichwani na mgongoni na walimu wanne huku wakiniambia nisali sala yangu ya
mwisho kutoka saa nne asubuhi hadi saa 10 jioni.
“Nilikuwa nikiishi maisha ya kuomba omba mitaani ili nipate
fedha kwa mahitaji ya shule nikiwa nimevaa sare za shule nikawa naitwa ‘malaya
aliyejificha kwenye unifomu za shule’ iliniuma sana,”alisema Consoler.
Alisema baada ya kipigo hicho amekuwa na maumivu makali
ya kichwa na mgongo ambayo humfanya
asiweze kufanya kazi zake kwa ufanisi kwani muda mwingi huutumia kwa kulala tu.
Anaomba kwa yeyote atakayeguswa na matatizo yake amsaidie
kwa hali na mali ili akapate tiba na anayetaka kuwasiliana nae kwa namba za
simu ambazo ni 0715025565 na 0787025565.
Alisisitiza kuwa kwa
sasa amewasamehe wote waliomfanyia anachohitaji ni kutibiwa ili arudi katika
hali yake ya kawaida.
Aidha aliwataka wototo wa kike wasinyamaze wanapokutana na
manyanyaso ya aina yoyote yale ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa kwa majirani.
Kwa sasa asasi ya New Hope For Girls inawahudumia watoto wa
kike 147 ambao wanatoka katika mazingira magumu na kati yao 24 wanaishi pamoja
na mlezi huyo.
mwisho