DIWANI wa kata ya Mbagala, Manispaa ya Temeke,jijini Dar es
Salaam,Aggrey Kayombo amewataka viongozi wa dini kufundisha maadili ya
kitanzania hasa kwa vijana ambao kwa sasa wanakumbwa na wimbi la utandawazi na
kupoteza asili yao.
Kayombo aliyasema hayo juzi katika msikiti wa Salama uliopo
kizuiani Mbagala wakati akizungumza na viongozi wa Bakwata wa kata hiyo katika
hafla fupi ya kuwaaga na kuwashukuru kwa ushirikiano waliouonyesha katika
kipindi cha uongozi wake.
“Viongozi wa dini mna nafasi kubwa katika kutoa elimu ya
maadili kwa vijana na watoto ili waweze kuwa na tabia njema na kioo cha taifa
la kesho hivyo basi timizeni wajibu huu, ” alisema Kayombo.
Alisema kuwa walimu wa dini wana nafasi kubwa kuliko
viongozi wa siasa katika ulinzi wa amaani na utulivu kutokana na mafundisho yao
ya kumjua Mungu na kutambuana wenyewe ambayo huleta hofu ya Mungu na hivyo
kuleta amani ya nchi.
Aidha aliwaomba kuwapa ushirikiano wale wote wanaoomba
kugombea uongozi kwa ngazi mbalimbali kwani wako sahihi kwa mujibu wa sheria na kanuni za
nchi.
“Wazee wangu nawaomba ushirikiano mlionipa mimi mpeni
yeyote atakaechaguliwa kuwa kiongozi katika nafasi yoyote
hii ndio demokrasia,” alisema Kayombo.
Awali akisoma risala kwa niaba ya viongozi hao, katibu wa
Bakwata wa kata ya Mbagala, Saidi Msati alisema Diwani huyo aliweza
kuwaunganisha viongozi wa dini mbalimbali ndani ya kata hiyo na kuleta
mshikamano, umoja na amani ambayo imedumu muda wote alipokuwepo madarakani.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni