Jumatano, 8 Julai 2015

TAKATAKA SASA KUTENGENEZWA MBOLEA



HALMASHAURI ya Manispaa ya Kinondoni imeingia makubaliano na Jiji la Humburg  la Uingereza kujenga mtambo wa kuchakata taka katika eneo la Mabwepande.
Ujenzi wa mtambo huo utagharimu    Sh bilioni 3.5.
Hayo yalielezwa Dar es Salaam jana na Meya wa Manispaa hiyo, Yusuph Mwenda wakati wa uzinduzi wa soko la wafanyabiashara wadogo Sinza.
“Tayari tumepata kiwanda ambacho tutakitumia kuchakata taka za ‘organic’ ambazo zitatengenezwa mbolea ambayo tutaitumia kwa   matumizi mbalimbali.  Mradi huo tunatarajia utatengeneza ajira zaidi ya 1,000,” alisema Mwenda.
Akizindua soko hilo, alisema litasaidia kupunguza idadi ya wafanyabiashara wasiokuwa na maeneo maalum ikizingatiwa lina vizimba 512.
“Kunzia KESHO mnaruhusiwa kuanza kufanya biashara kwa sababu soko hili tumelijenga si mapambo tunataka kukabiliana na changamoto ya wafanyabiashara kutokuwa na maeneo maalum pamoja na ukosefu wa ajira.  Vipo vizimba 512 kwa maana hiyo tutapunguza kwa kiasi changamoto hii,” alisema.
Alisema manispaa hiyo pia imeanza ujenzi wa soko jingine kubwa eneo la Mburahati litakalogharimu Sh bilioni 1.8  kwa ajili ya   wafanyabiashara wa bidhaa ndogo ndogo.
  Meneja msimamizi wa soko hilo, Elichilia Mushi alisema   limejengwa kwa mfumo wa kisasa ili kuboresha huduma za wafanyabiashara hao.
“Tumepanga wafanyabiashara kulingana na aina ya bidhaa aliyonayo, lengo letu ni kuwavutia watu wengi zaidi na kuboresha huduma ya soko hili kuwa tofauti na mengine.  Pia tunazingatia suala la usafi,” alisema.
Alisema katika kutekeleza hilo zimewekwa sheria, kanuni na utarabu ambao utawasaidia kuboresha usafi ndani ya soko hilo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni