Jumanne, 14 Julai 2015

TAHADHARI YATOLEWA KWA WANUNUA ARDHI



MKUU wa Wilaya ya Mkuranga, mkoani Pwani Abdallah Kihato amewatahadharisha watu wanaokwenda kununua ardhi katika wilaya yake hasa vijiji vinavyopakana na Ilala kuwa makini na matapeli wanaovamia maeneo hayo.
Akizungumza na Blog hii jana ofisini kwake, Kihato alisema kumeibuka malalamiko mengi hasa katika kijiji cha Tambani kuwepo matapeli wanaovamia mashamba yasiokuwa yao na kukata viwanja na kuuzia watu kwa madai kuwa eneo hilo liko Ilala.
“Ni muhimu kwa wanunuzi kufuata taratibu zote za ununuzi wa ardhi kwa kuwashirikisha viongozi wa kijiji ili kuthibitisha kama muuzaji ni eneo lake,” alisema kihato.
Alisema wanazo idara za ardhi kwa kila ngazi na upo utaratibu kwa mnunuzi na muuzaji kufika ofisi za kijiji kutambuliwa.
“Wakati mwingine watu wetu wanaingia katika migogoro hiyo kutokana na kuwa na haraka, wanakosa udadisi hawawezi hata kujiridhisha kwa majirani,” alisema Kihato.
Alisema wamekubaliana na Mkuu wa Wilaya ya Ilala kuwa na kikao cha pamoja cha kamati za ulinzi na usalama kutokana na lawama nyingi za uvamizi kuripotiwa kutokea maeneo ya Wilaya hiyo.
“Migogoro mingi imetokana na kuharibiwa kwa ramani ya mwaka 1974 inayoonyesha mipaka ya wilaya hizi mbili,” alisema.
Alisema hati nyingi zimeandikwa kuwa kijiji cha Tambani kiko Ilala kitu ambacho si kweli hakuna mtaa huo katika wilaya hiyo.
Migogoro hiyo ya ardhi katika eneo hilo imesababisha watu wawili kupoteza maisha yao kutokana na mapigano kati ya wakazi na jamii ya Wakurya wanaodaiwa kuvamia maeneo ambayo si ya kwao.
mwisho

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni