MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Mkuranga imemwachia
huru askari polisi mwenye namba 3949 Cpl Innocent Haule, ambaye alikuwa akikabiliwa
na shitaka la kumpiga na kumjeruhi Abdul Jongo kwa kutumia rungu.
Askari huyo aliachiwa huru juzi na mahakama
hiyo kutokana na upande wa Jamhuri kushindwa kuthibitisha mashitaka dhidi yake
pasi kuacha shaka yoyote.
Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mkazi Agnes
Mchome alikiri kuwepo mahakamani hapo ushahidi uliothibitisha kijana kupigwa na
askari huyo.
“Kutokana na ushahidi wa daktari umeonyesha kweli alipigwa
kichwani na kitu kizito na kumsababishia majeraha,” alisema Mchome.
Alisema katika ushahidi wote uliotolewa mahakamani hapo
hakuna sehemu iliyoonyesha kuwa mshtakiwa alikuwa na dhamira ya kumpiga na wala
hakuna zana iliyoletwa mahakamani na kudaiwa kutumiwa na mshtakiwa.
“Upande wa Jamhuri umeshindwa kuthibitisha
mashitaka dhidi ya mshitakiwa pasi kuacha shaka yoyote, hivyo mahakama
inamwachia huru mshitakiwa,” alisema Hakimu huyo.
Awali akisoma shitaka hilo mbele ya hakimu mkazi, wakili wa
serikali Debora John alidai kuwa mnamo disemba 26, 2010 katika eneo la Vikindu
wilayani humo, mshtakiwa alitenda kosa hilo kwa kumpiga na rungu Abdu Jongo na
kumsababishia jeraha kichwani.
Hukumu hiyo iliacha maswali mengi hasa kwa ndugu wa
mlalamikaji kwa kuwa hakimu alikiri kuwepo ushahidi ulioonyesha dhahiri
kupigwa.
mwisho
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni