Jumatano, 8 Julai 2015

MFUMUKO WA BEI WAENDELEA KUPAA



MFUMUKO wa bei wa Taifa kwa mwezi juni, 2015 umeongezeka hadi asilimia 6.1 ukilinganisha na asilimia 5.3 kwa Mei mwaka huu.
Hii inamaanisha kuwa kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishia mwezi Juni 2015 ikilinganishwa na kasi iliyokuwepo kwa mwaka ulioishia Mei 2015.
          
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii, Ephraim Kwesigabo alisema ongezeko hilo limechangiwa na kuongezeka kwa bei za baadhi ya vyakula na zisizo za vyakula katika kipindi kilichoishia juni mwaka huu.

Alisema fahirisi (kipimo) za bei zimeongezeka hadi 158.12 Mei, 2015 kutoka 148.98 juni, 2014.

"Mfumuko wa bei umeendelea kuongezeka pia kutokana  na ongezeko la bei za mafuta hasa petrol kwa asilimia 5.2 na diesel kwa kwa asilimia 4.5.


"Mfano mwenendo wa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula kama zilizoonyesha kuongezeka mwezi juni 2015 zikilinganishwa na bei za juni,2014 ni pamoja na mchele kwa asilimia 31.5, mahindi kwa asilimia 8.1,unga wa muhogo asilimia 3.7, nyama asilimia 3.1, samaki asilimia 12.0 na maharage asilimia 11.6. alisema Kwesigabo.

Kwesigabo alisema mfumuko wa bei kwa bidhaa  zisizo za vyakula zilizochangia kuongezeka kwa kwa mfumuko wa bei mwezi juni 2015 zikilinganishwa na bei za juni 2014 na pamoja na bei za mavazi wanaume kwa asilimia 3.6, mavazi ya wanawake asilimia 2.6,vyakula kwenye migahawa kwa asilimia 3.5, na huduma za malazi kwa asilimia 3.1.


"Mfumuko wa bei kwa kipimo cha mwezi umeongezeka kwa asilimia 0.2 mwezi juni, ukilinganisha na 0.4 kwa mwezi mei mwaka huu mwaka huu," alisema.

Alisema uwezo wa shilingi 100 katika kununua bidhaa na huduma umefikia shilingi 63 na senti 24 mwezi juni, mwaka huu kutoka Septemba, 2010 ikilinganishwa na shilingi 63 na senti 35 mwezi Mei mwaka huu.

Alisema hata hivyo mfumuko wa bei nchini una mwelekeo unaofanana na baadhi ya nchi za Afrika Mashariki ambapo kenya umeongezeka kwa asilimia 7.03 kutoka asilimia 6.87 mwezi mei 2015 na Uganda kubaki 4.90 kama ilivyokuwa mwezi mei mwaka huu.

Aidha amewaomba wananchi kutoa ushirikiano wa dhati kwa ofisi za takwimu za mikoa wakati wa ukusanyaji wa takwimu mbalimbali kwa lengo la kutoa taarifa zilizo sahihi kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni