MANISPAA
ya Ilala imesema itawachukulia hatua watu wanaogawa viwanja kwa wamachinga
katika eneo la jangwani kwa madai kuwa wameruhusiwa na uongozi kufanya hivyo.
Akizungumza
na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa manispaa hiyo,
Isaya Mngurumi alisema hawajamruhusu mtu yeyote kugawa viwanja bali
waliwaruhusu kupanga chini bidhaa zao kama wanavyofanya katika mitaa ya
kariakoo.
“Nimetuma
timu kuwatafuta watu wanaogawa maeneo hayo kwani waliokimbilia huko si walengwa
ni wajanja wachache tu,” alisema Mngurumi.
Alisema
walikaa na uongozi wa manispaa ili kutafuta eneo la wafanyabiashara wadogo
ndipo wakateua jangwani kuwa sehemu ya muda wakiwa bado wanaandaa masoko rasmi.
“Tumechagua
jangwani upande wa kushoto wa barabara kama unaelekea kigogo kama sehemu ya
muda kabla hatujaweka miundombinu ya vyoo wamevamia na kugawana bila ruksa ya
manispaa,” alisema Mngurumi.
Alisema
upande wa kulia wa barabara ni eneo la huduma za kijamii hasa uwanja wa mikutano
ya hadhara na stendi ya mabasi yaendayo kasi.
Aidha
alisema wako katika mkakati wa kujenga masoko ambayo yatawasaidia
wafanyabiashara hao wadogo kuwa katika maeneo ya kudumu ya kufanyia shughuli
zao.
Aliyataja
masoko hayo kuwa ni Kisutu, Buguruni na Mchikichini ambapo wanaongea na wadau
mbalimbali ili kupata mikopo kwa ajili ya ujenzi.
“Tumeingia
mkataba na Benki ya TIB ili kujenga soko la kisutu kwa gharama ya sh. bilioni
11,” alisema.
mwisho