Alhamisi, 4 Juni 2015

SIKU YA MTOTO DUNIANI KUAZIMISHWA DAR KWA KUZINDUA CD YA THAMANI YETU LEO



SHIRIKA lisilo la kiserikali la Women In Society(WoInSo)  inatarajia kutambulisha programu maalumu itakayotoa elimu kuhusu afya, maisha na mazingira ya malezi ya mtoto ndani ya jamii.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa bodi ya shirika hilo, Juliana Madereke alisema utambulisho huo utaambatana na sherehe za siku ya mtoto duniani zitakazofanyika juni 6 mwaka huu Millennium tower ambapo Mkurugenzi wa Chama Cha Uzazi na Malezi Bora Tanzania(UMATI), Lulu Ng’wanakilala anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Madereke alisema elimu hiyo itawasaidia watoto kujitambua pamoja na kuwashawishi wazazi kubadili tabia ambazo zinamfanya mtoto asifikie malengo yake.
“Mtoto anafanyishwa kazi ambazo si sawa na umri wake na jamii inaangalia tu bila kuhoji kwanini mzazi anafanya hivyo,” alisema Madereke.
Alisema wameandaa filamu itakayogawiwa bure nchi nzima iitwayo thamani yetu leo yenye maudhui ya ukatili wanaofanyiwa watoto na wanajamii.
Alisema jamii iondokane na kauli ya zamani ambayo watoto wanaambiwa kuwa kila anachosema na kufanya mkubwa ni sahihi kitu ambacho humfanya aogope kusema anapotendewa mabaya.
Nae Mwenyekiti wa Nidhamu, Zenais Mtebe aliiomba serikali kutoa ushirikiano na kuwapa kipaumbele watoto ili kuwasaidia katika matatizo yanayowakabili.
“Jamii ione thamani ya mtoto na kumuona hata mtoto wa mwenzako nae ni wako na kuvunja ukimya majumbani na kuzungumza yale yanayotokea kwa watoto,” alisema Mtebe.
    

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni