CHAMA cha Taifa
cha Alliance For Tanzania Farmers Party (AFP) kimemshauri msajili wa vyama vya
siasa Tanzania, Jaji Francis Mutungi kujiepusha kuingilia migogoro ya ndani ya
vyama vya siasa kutokana na kuwa inaonekana kukuza zaidi migogoro.
Akizungumza
na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Habari na Uenezi
Taifa wa chama cha AFP, Mwarami Uwesu, alisema kuwa msajili wa vyama anatakiwa
kuacha kuingilia migogoro ya ndani ya vyama vya siasa na badala yake anatakiwa
kuhimiza demokrasia.
Alisema Kamati
Kuu ya AFP ilikutana machi 13 kwenye ofisi za makao makuu ya chama zilizopo
Temeke na kuamua kumsimamisha Katibu Mkuu , Rashid Rai kutokana na kushindwa
kutekeleza majukumu yake ndani ya chama uamuzi ambao msajili wa vyama anaupinga
na kudai kutotambua.
Alisema maamuzi
ya msajili ya kutotambua kusimamishwa kwa katibu mkuu wa chama hicho
yanaingilia katiba yao ibara ya 10.a(3) inayosema kuwa kiongozi anaweza kukata
rufaa kwa kikao cha juu iwapo hakuridhika na uamuzi wa kikao cha chini dhidi
yake.
“Kutokana na
maelekezo ya katiba yetu chama hakikubaliani wala hakijaridhishwa na maamuzi
yaliyofanywa na ofisi ya msajili hivyo tumeamua kumpinga kwa kumuandikia barua
yenye kumbukumbu namba. A.F.P/HQ/08/F1/2015 ambayo tuliiandika juni 11 na
kumuomba kupitia ofisi yake kushughulikia shauri hilo kwa umakini,” alisema
Uwesu.
Alisema katika
barua hiyo pia walimtaka kuzingatia taratibu za ofisi yake pamoja na kuheshimu
katiba ya chama chao kutokana na kuwa bado wana nafasi ya kuweza
kulishughulikia suala hilo kwenye vikao vya halmashauri kuu pamoja na mkutano
mkuu kwa kuwa katibu huyo hakufukuzwa moja kwa moja.
“Maamuzi ya
kumsimamisha Katibu Mkuu yalifanywa na Kamati Kuu ya utekelezaji ya AFP Taifa
kutokana na kuwa ndio chombo kinachofanya shughuli zote za chama kwa mujibu wa
katiba yetu ibara ya 16.8(d) na 16.8(f) lakini bado Rashid anatambulika kama
katibu mkuu wa chama,” alisema Uwesu.
Aidha alisema
kuwa Kamati Kuu ya utekelezaji imeanza kutoa fomu kwa wagombea wa ngazi zote
katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba na mwisho wa kutoa fomu hizo
utakuwa Juni 30.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni