Jumanne, 16 Juni 2015

DK. GHARIBU BILALI: MSIBA WA MUFTI SIMBA NI WA KITAIFA



MAKAMU wa Rais Dk. Gharib Bilal ameutangaza msiba wa Sheikh Mkuu wa Tanzania, Issa Shaaban bin Simba uliotokea juzi asubuhi katika hospitali ya TMJ kuwa wa kitaifa.
Kiongozi huyo aliyasema hayo jana, Dar es Salaam kwa niaba ya Rais Jakaya Kikwete kwenye viunga vya msikiti wa Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata) kwa ajili ya kumsomea dua marehemu Mufti.
“Msiba wa Mufti ni wa kitaifa na nadiriki kusema kuwa serikali imepoteza kiungo muhimu baina yake na waislamu katika suala la kudumisha amani,”alisema.
Dk. Bilal alisema kuwa Mufti Simba alikuwa kiongozi tegemeo katika uhamasishaji wa amani na maendeleo ya binadamu kwa watu wa imani tofauti tofauti hapa nchini.
Makamu huyo wa Rais alimuelezea Mufti Simba kama mtu ambaye hakuwa mbinafsi, mbaguzi, hakuwa mtu mwenye makuu na wala hakuwa mwenye majivuno na kujiona.
Naye Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba aliyezungumza kwa niaba ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) amemuelezea Mufti kama mtu wa watu ambaye anastahili kukumbukwa kwa kufanya mazuri aliyoyaacha.
Mwingine aliyemzungumza Mufti katika viwanja hivyo vya Bakwata alikuwa Mwenyekiti wa Kampuni ya IPP Abraham Mengi alisema kuwa atamkumbuka kama rafiki na mtu aliyekuwa mnyenyekevu.
“Hata baada ya kupata uongozi wa juu hakubadilika, aliwapenda watu kuliko alivyojipenda mwenyewe, Sheikh Mkuu amefariki kimwili lakini mawazo yake yataendelea kuishi katika roho yangu kutokana na namna alivyokuwa akijitolea kuwasaidia watu,” alisema.
Mussa Zungu alitumia muda huo kwa niaba ya Spika na Bunge la Tanzania kwa kuwapa pole waislam, watanzania na familia ya marehemu na kuwaomba waendeleze wema na amani aliyokuwa akiuhubiri marehemu.
Naye Mkurugenzi wa Msama Promotion Alex Msama alimuelezea Sheikh Simba kama mtu wa watu, aliyekuwa akipinga kufanyiwa uonevu watu na alikuwa akijaribu kuwaunganisha waislam na wakrito hivyo kuondoka kwake imekuwa pengo kubwa.
Waliohudhuria katika dua hiyo ni pamoja na Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi, Salim Ahmed Salim, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Zanzibar Mohammed Abood,  Katibu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Dk Wilbrod Slaa, Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe.
Wengine ni Sitti Mwinyi, Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kingunge Ngombare Mwiru, mabalozi wa nchi za Sudan, Comoro, Palestina na Iran.   
         



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni