KAMPUNI ya uwekezaji ya wazawa(NICOL), imeanza uchunguzi wa
hasara ya shilingi bilioni 10 iliyopata baada ya kufanya uwekezaji mbaya katika
kampuni mbili tofauti.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es
Salaam, Mwenyekiti wa NICOL, Gideon Kaunda alisema uchunguzi huo utafanyika
ndani ya wiki mbili na baada ya ripoti kukabidhiwa watawafungulia kesi
mahakamani wote waliosababisha hasara hiyo.
Alisema hadi kufikia Disemba 31, 2009, kampuni hiyo ilipata
hasara hiyo kutokana na kuwekeza katika kampuni ambazo baadaye zilifilisiwa na
benki zilizokuwa zikizidai.
“NICOL iliwekeza Dola za Marekani Milioni mbili(sawa na
shilingi bilioni nne) katika kiwanda cha kutengeneza dawa kilichopo Moshi,
mkoani Kilimanjaro ambacho kilikuwa kimekopa katika benki ya Barclays na baada
ya kushindwa kulipa deni hilo benki ilikitaifisha na kusababisha fedha hizi
kupotea,” alisema Kaunda.
Alisema katika uwekezaji mwingine NICOL iliwekeza shilingi
bilioni tatu katika kiwanda cha samaki kilichopo Mwanza na baadaye kukiongezea
shilingi bilioni tatu ambacho nacho kilikopa fedha katika Benki ya Maendeleo ya
Afrika(ADB).
“Baada ya uwekezaji wa mwaka mmoja kilishindwa kulipa deni
hilo lililosababisha kufilisiwa na benki hiyo hivyo kupoteza fedha hizo,”
alisema Kaunda.
Alisema
pia wamebaini kuwa kutokana na uzembe ulifanyika katika kipindi cha uongozi wa
Mwenyekiti wa zamani, Felix Mosha umesababisha kampuni tanzu ya Tanzania Meat
Company ltd na ile ya Mwanza kufanya ubadhilifu.
“Mbali
na kuwapo kwa matumizi mabaya ya fedha pia kodi za serikali na michango ya watumishi
katika mifuko ya hifadhi za jamii haikuwa ikipelekwa hivyo kuongeza madeni,”
alisema Kaunda.
Alisema katika
uchunguzi huo pia wataangalia upya mikataba ya kampuni za nje zinazonunua nyama
iliyoingiwa na TMC kutokana na kuwa na mapungufu mengi.
Aidha
Kaunda alisema mapema mwakani wataanza kuwekeza tena katika soko la hisa baada
ya kumalizika kwa migogoro ya uongozi iliyokuwapo awali.
mwisho
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni