Alhamisi, 15 Desemba 2016

Platinum Credit kudhamini uchunguzi saratani ya shingo ya kizazi

KAMPUNI ya Platinum Credit Ltd kwa kushirikiana na Hospitali ya mkoa ya Mwananyamala watatoa bure huduma za uchunguzi wa saratani ya shingo ya kizazi kwa wanawake jijini Dar es Salaam.
 Akizungumza na waandishi wa habari jana Meneja Mauzo wa kampuni hiyo, Lufunyo Gideon alisema wameamua kufadhili uchunguzi huo ikiwa ni zawadi ya sikukuu ya Chrismas na kurudisha kile walichokipata kwa jamii.
Alisema uchunguzi huo utafanyika katika hospitali ya Mwananyamala iliyopo Kinondoni jijini Dar es Salaam kuanzia kesho hadi Disemba 21, mwaka huu.
“Tunawaomba wanawake wajitokeze kwa wingi katika kufanyiwa uchunguzi ili waweze kutambua afya zao mapema na kupata ushauri,” alisema Gideon.
Naye Mganga mfawidhi wa Hospitali ya Mwananyamala Dk.Daniel Nkungu alisema ni fursa kwa wanawake kujua afya zao ili kama wana ugonjwa huo wapate matibabu mapema.
“Tatizo lililopo kwa sasa ni watu kuchelewa kugundua dalili za awali za ugonjwa huo hivyo kugundulika ukiwa katika hatua mbaya ambayo mara kadhaa umekisababisha vifo,” alisema Dk.Nkungu.
Alisema wahudumu wa hospitali hiyo wamejipanga vizuri kuendesha uchunguzi huo hivyo wasiogope kwa kudhani kutakuwapo na foleni kubwa.

“Niwaombe wanawake wajitokeze kwa wingi kupima kwa kuwa tumejipanga vizuri katika kuwapokea na kuwafanyia uchunguzi kwa haraka,” alisema Dk.Nkungu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni