Jumatano, 7 Desemba 2016

kampuni yadai kuidai TPA Bil.2

KAMPUNI ya Baga Investment imeshindwa kulipa kwa wakati posho za baadhi ya wafanyakazi wake kwa madai ya kuidai Mamlaka ya Bandari Tanzani(TPA) shilingi bilioni 2.

Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni hiyo, Jumbe Moshi, aliyasema hayo jana baada ya kuwapo kwa malalamiko ya baadhi ya wafanyakazi wa kampuni hiyo ambao wanalipwa kwa siku kudai kutolipwa posho zao kwa siku 23.
Alisema ni zaidi ya miezi mitatu sasa TPA imeshindwa kuwalipa fedha hizo hivyo kushindwa kulipa madeni yanayowakabili yakiwamo ya Benki.

“Kuchelewa kulipwa kwa wafanyakazi wetu kunatokana na TPA kushindwa kuilipa kampuni kwa miezi mitatu jambo ambalo linarudisha nyuma utendaji wa kampuni.

 “Hali hii imetuweka katika wakati mgumu kutokana na kampuni kudaiwa na baadhi ya Benki hali inayofanya tushindwe kulipa na kujiendesha,” alisema Moshi.
 Moshi alisema kuwa kampuni hiyo iliingia mkataba na TPA wa kufanya kazi za ufundi wa kutengeneza maboti, magari na udereva wa folk ambapo kampuni hiyo ilianza kazi hizo mwaka 2012.
 “Tunakutana nao mara kwa mara na wanatuomba radhi kwa kututaka tuvute subira mambo yakikaa sawa watatulipa,”alisema Moshi.

Akizungumzia malalamiko ya wafanyakazi hao, Moshi alisema kampuni hiyo imejitahidi kulipa posho za wiki iliyopita lakini juhudi zinaendelea kufuatilia fedha wanazozidai TPA ili waweze kuwalipa fedha zao zote.

Aidha Moshi alisema wafanyakazi hao licha ya kulipwa kwa siku lakini kutokana na makubaliano yao kila mmoja anapofanikiwa kuingia kazini lazima anapelekewa makato yake NSSF.

Awali baadhi ya wafanyakazi wa Kampuni hiyo ya Baga Investment, walidai kuwa hawajalipwa posho hizo kwa siku 23 sasa.

Mmoja wa wafanyakazi hao ambaye hakutaka kuandikwa gazetini alisema kila walipouliza walijibiwa kwamba chimbuko la kuchelewa huko kumesababishwa na TPA  ambayo haijailipa kampuni hiyo kwa zaidi ya miezi mitatu.

Akizungumzia malalamiko hayo, Msemaji wa Bandari Janet Ruzangi alisema madai hayo hayana ukweli kwa sababu kampuni hiyo inalipwa kwa wiki.
“Sijui mkataba wao na TPA unasemaje lakini mara nyingi malipo yao yanakuwa kwa wiki au mwezi kwa sababu Baga Investment mpaka wameingia mkataba na kuendesha shughuli hiyo inamaana walikuwa wanazo fedha za kutosha na siyo mpaka walipwe,” alisema Ruzangi.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni