Jumapili, 4 Desemba 2016

QUALITY WAISOMA


KAMPUNI ya Quality Group inayomilikiwa na mfanyabiashara Yusuf Manji imeondolewa katika jengo iliyokuwa ikilikalia lililoko kiwanja namba 189/2 barabara ya Nyerere, jijini Dar es Salaam kutokana na deni la malimbikizo ya ya pango la shilingi bilioni 13.
Kampuni hiyo inadaiwa kiasi hicho cha fedha kutokana na kulimbikiza deni hilo kwa miaka mingi tangu ipangishwe na mmiliki wa jengo hilo ambaye ni Mfuko wa Pensheni wa PSPF.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Meneja wa Operesheni wa kampuni ya Udalali ya Yono ambao ndio walipewa zabuni ya kuiondoa kampuni hiyo, Atukuzwe Muhugo alisema kazi hiyo imefanikiwa baada ya kutoa notisi ya masaa 24 kuitaka iondoke.
Alisema notisi hiyo iliisha alfajiri ya jana ndipo walipofika kuiondoa kwa nguvu lakini wafanyakazi walitii sheria na kuanza kutoa mali zao.
“Wafanyakazi wa Quality Group hawakuwa wajeuli wametii amri bila shuruti jambo lililoturahisishia kazi yetu,” alisema Atukuzwe.
Alisem jengo hilo litakuwa chini ya Yono mpaka hapo litakapokabidhiwa kwa PSPF.
Aliyataja ofisi zilizoondolewa kuwa ni Chief Exercutive officer of Quality Group Company LTD, Gaming Management Ltd, Q Consult Ltd, Quality Logistics Company Ltd na International Transit Investment Ltd .
Mmoja wa mahusika katika kampuni hiyo ambaye hakutaka kutaja jina lake alipotakiwa kuzungumzia tukio hilo alisema hajajiandaa kuongea na wanahabari na hivyo kuwaomba wafike leo saa nane mchana ndipo ataongea.
“I don’t have suit, come tomorrow I will be ready to talk to you, how could I talk to you without wearing suit? Come tomorrow after lunch on 2  (siwezi kuzungumza bila kuvaa suti hivyo nawaomba mje kesho saa nane mchana ),” alisema.
Ilishuhudiwa magari aina ya Isuzu yenye namba za usajili T385 DAB na T620 DCC yakipakia vitu na kupeleka sehemu ambayo haikujulikana mara moja.
Uamuzi wa kuindoa Quality Group katika jengo hilo umetokana na kushindwa katika kesi namba 33 ya mwaka 2009 iliyofungua kampuni hiyo  katika mahakama kuu, Divisheni ya ardhi ikipinga kuondolewa.
Kesi hiyo ilimalizika Novemba 24, mwaka huu kwa mahakama kumpa haki mmiliki wa jengo hilo PSPF kutafuta dalali wa kumwondoa Quality Group.

Jaji aliyetoa hukumu hiyo aliamuru kuondolewa kwa Kampuni hiyo  na kuiacha PSPF kama mmiliki wa jengo hilo na ndipo Yono walipopewa zabuni ya kwenda kumwondoa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni