Jumatatu, 22 Juni 2015

TANZANIA KWA UBUNIFU KIBOKO



“TANZANIA ni wabunifu na tunahitaji ubunifu kwa maendeleo ya nchi lakini sio ubunifu huu wa ovyo,” hiyo ni kauli iliyotolewa kwa masikitiko na Rais Jakaya Kikwete alipokuwa akizungumza na wakuu wa mikoa na wilaya alipokuwa Singida hivi karibuni.
Kauli hii ya Rais ilikuja baada ya baadhi ya watanzania kujaribu kubadilisha matumizi ya vitu kuwa wanavyotaka wao.
 Inawezekana hali ya umaskini wa watu wengi ndio hupelekea baadhi ya watu kubuni njia ambazo zinawasaidia kupata vitu vya gharama nafuu tofauti na uhalisia.
Akiwa Singida Rais anasikitishwa na tabia ya baadhi ya watu wanaotumia vyandarua ambavyo vimegawiwa bure na Serikali kwa kila kaya nchini kwa lengo la kutokomeza malaria na wao kubadilisha lengo lililokusudiwa kwa kufugia kuku ama kuvulia samaki na wengine wakidiriki kujengea msalani.
 “Watu wetu wa ajabu sana, tumegawa vyandarua bure ili sote tuondokane na tatizo la malaria, lakini nasikitika ninavyosikia kuwa wengine wanavitumia kufugia kuku.
“Kweli Tanzania inahitaji ubunifu, lakini siyo ubunifu wa namna hii wa ovyo, tuache kutumia vyandau kufugia kuku, tuvitumie kama ilivyokusudiwa.” Anasema Kikwete.
Vidonge vinavyotibu maradhi mbalimbali
Dawa za kuchochea uchungu kwa wajazito zikiwamo ‘misoprostol’ , ‘oxytocin’ , `Mifecon-Mkit’ zinazopatikana kiholela kwenye maduka ya dawa zimekuwa zikitumika kwa utoaji mimba holela ambao hufanyika bila hofu yoyote.
Vidonge hivyo hupanua shingo ya kizazi na kusababisha hewa kupita kwenye nyumba ya uzazi na kubomoa ukuta wa tumbo la uzazi na kuharibu mimba.
Misoprost -200 maarufu kama ‘miso’ ni vidonge vinavyodaiwa kubadilishwa matumizi yake ya awali na kuwa dawa za kutolea mimba.Jijini Dar es Salaam matumizi ya dawa hii yameongezeka kwa kutolea mimba hasa kwa baadhi ya wanafunzi na wafanyabiashara za ngono.
Dawa ya ‘mkit’ ambalo katika mahojiano na baadhi ya wanafunzi na wafanyabiashara ya ngono wamekuwa walisifia kwa kudai inatoa mimba yenye umri wowote hata pale ‘miso’ inaposhindwa.
 Kwa upande wa dawa ya ‘oxytocin’ watumiaji kuchomwa sindano na kurudi nyumbani kusubiri mimba iharibike.
Tembe nyingine zinazotumiwa ni ‘arzithromycin-500’ ambazo huingizwa sehemu za siri na nyingine humezwa. kazi ya dawa hii si kuharibu mimba bali ni kutibu kama kifua, magonjwa ya zinaa na kukausha vidonda vilivyotokana na kushambuliwa na vimelea.
Dawa hizi hutumika kwa maelekezo yanayotolewa na wahudumu wa maduka ya dawa, wahudumu wa afya wasio na maadili na madaktari ‘vishoka’ mitaani.
Baadhi ya wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu wanakiri kuwa dawa hii inawasaidia lakini wengine walisema si wakati wote kwani wapo waliodai waliitumia lakini badala ya kuharibu iliikomaza mimba.
Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam(UDSM) Elizabeth  Joseph anasema yeye hajawahi kutumia vidonge hivyo lakini rafiki zake hununua kwenye maduka ya dawa na kutumia kutoa mimba.
Matumizi ya dawa ya malaria aina ya Metakelfin yamebadilishwa na sasa ni kutengeneza kipodozi cha kurembesha nywele. Utafiti uliofanywa hivi karibuni na shirika lisilo la kiserikali la Envirocare linalojihusisha na mpango wa  kupunguza madhara yatokanayo na bidhaa za vipodozi kwa binadamu na mazingira, umebaini dawa ya malaria ni aina mojawapo ya kemikali inayotumika kienyeji  katika kutengeneza kipodozi cha kurembesha nywele.

Imeripotiwa kuwa baadhi ya wafugaji wa Mkoa wa Mbeya wanatumia dawa za kupunguza makali ya UKIMWI (ARVs) kwa ajili ya kunenepesha mifugo yao.
Kwa mara ya kwanza habari hizo zililipotiwa na Gazeti hili Toleo Na. 4990  Januari11 , 2010.
 Dawa hizo zinadaiwa kukuza haraka na kunenepesha mifugo kama Nguruwe, ng’ombe, kuku na wengineo.

Inadaiwa kuwa dawa ya kutibu magonjwa ya mifupa indomethacin maarufu kama indocid imekuwa ikitumika kama sumu ya kuulia panya.
“Indocid ni sumu nzuri sana kwa panya, ukiichanganya na chakula panya wakila wanakufa,” anasema Asia Mohammed ambaye ni mkazi wa Uzuri ,Manzese. 
Mbolea za mazao
Baadhi ya wafugaji wa Wilaya ya Kiteto mkoani Manyara, wanatumia mbolea ya kupandia na kukuzia mazao kulishia mifugo yao kwa madai kuwa huinenepesha. Hayo yalielezwa na Ofisa Tarafa ya Makame, Ibrahim Ole Mario alipokuwa akizungumza katika mafunzo ya wenyeviti 25 wa vikundi vya wakulima wa Kiteto.
Kondom za kike
 Huko Rukwa baadhi ya wanawake mkoani humo wamekuwa wakitumia kondomu za kike kwa kuzivaa kama urembo wa bangili.

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEj9OCiSiDpKSzRPXc_q_A1pRVVKYOt2xK20xAnA7XJy2Q0aCNWJFJNHWtdKL9pAgaeKyowKLL7lwDtNMYJ6iFoCu3xIXEcjVWTV_n955uzHK1YU1GQQVo3KRgkidaLi_6OMpDYssvxWQsIq/s1600/KINGA.jpg
Matumizi ya sarafu
SARAFU mpya ya shilingi 500 inadaiwa kutumiwa na baadhi ya watu ambao huinunua kwa Sh 2,500 na baadaye kuiyeyusha kwa ajili ya kutengenezea mikufu ya fedha (silver).
Benki kuu ya Tanzania ilitoa ufafanuzi kuhusu uyeyushaji wa sarafu hiyo. Apr 29, 2015 - 500 ni chuma na asilimia 6 ni Nickel, ameeleza Mkurugenzi wa Huduma za Kibenki katika Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Marcian Kobello.
 “Hakuna kabisa madini ya fedha katika sarafu ya sh. 500,” anasema Bw. Kobello na kuongeza kuwa haitegemewi kwamba mfanyabiashara yeyote anaweza kununua sarafu hiyo kwa bei ya juu kuliko thamani yake halisi.
Maji ya betri pamoja na jik
Jik na maji ya betri yamekuwa yakiripotiwa mara kwa mara kutumiwa kama malighafi na wataalamu wa kutengeneza mikorogo inayotumiwa na baadhi ya wanawake na wanaume kuchubua ngozi za miili yao.
 Utafiti uliofanywa hivi karibuni na shirika lisilo la kiserikali la Envirocare linalojihusisha na mpango wa  kupunguza madhara yatokanayo na bidhaa za vipodozi kwa binadamu na mazingira, umebaini kuwa maji ya betri pamoja na dawa ya kuondoa madoa (jik) vinatumika katika uandaaji wa mikorogo.
Mtafiti kutoka shirika hilo Issa Sen’genge anasema Swali lilikuwa kama kuna vitu vinavyotumika katika kutengeneza mchanganyiko wa kupaka kwenye ngozi au nywele, waliohojiwa walikiri kuchanganya, Metakelfin, Jik, maji ya betri na kemikali nyingine.
 Matumizi hayo ya hatari yanaweza kusababisha madhara makubwa kwa watumiaji.
Watanzania wamekuwa wakibadili matumizi ya vitu mbalimbali hata kama ni hatari kwa afya zao.

Alhamisi, 18 Juni 2015

BEI ZA FUTARI ZAPANDA



KUTOKANA na kuanza kwa Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, wafanyabiashara katika masoko mbalimbali wamepandisha bei za baadhi ya vyakula hali iliyoanza kuleta usumbufu kwa wananchi.
BLOG hii ilitembelea masoko kadhaa katika jiji la Dar es Salaam, leo na kubaini kuwa baadhi ya vyakula vimepanda bei  mara tu baada ya Mfungo kuanza.
Katika soko la Kisutu mfanyabiashara wa ndizi za kupika, Japhary Abdallah alisema bei ya bidhaa hiyo imepanda kutoka 15,000 hadi 30,000 kwa mkungu mmoja hivyo kumlazimu yeye kuuza sh.1,000  kwa ndizi tatu.
“Leo(jana) nimenunua mkungu  wa ndizi kwa sh. 30,000 kutoka kwa wakulima unategemea mimi nitauza kwa bei gani?,” alihoji Abdallah.
Mfanyabiashara wa mihogo na viazi katika soko la Mabibo, Juma Selemani alisema kiloba kimoja cha mihogo au viazi vitamu kilichokuwa kikiuzwa kwa sh.70,000 jana kimeuzwa kwa sh.110,000 na sh.100,000.
“Hali ya biashara leo ni ngumu kwa tunaofunga kutokana na vyakula hasa vinavyotumika kwa futari kuuzwa kwa bei kubwa na wakulima wanaoleta katika soko hili,” alisema Selemani
Katika soko la Kariakoo, mmoja wa wafanyabiashara wa Magimbi, Athanas Issa alisema alipata bidhaa hiyo maradufu ya bei ya awali.
“Awali magimbi mdima tulikuwa tukiyapata kwa sh.40,000 kwa kiloba cha kilo hamsini lakini leo tumepata kiloba hicho hicho kwa sh.80,000 tunauza fungu 3000, huku magimbi maji yaliuzwa kwa bei ya sh.90,000 na leo ni 150,000 kwa kiloba kikubwa nasi tunauza 4000 kwa gimbi moja,” alisema Issa.
Kwa upande wake Meneja mipango na shughuli za biashara wa soko la kariakoo, Mrero Mgheni alisema kupanda huko kwa baadhi ya vyakula kunatokana na mahitaji kuwa makubwa kuliko upatikanaji wake.
“Wiki ya kwanza ya mwezi wa Ramadhani vitu hupanda kutokana na uhitaji mkubwa tofauti na upatikanaji wake” alisema Mgheni.
Alisema mpaka Juni 14, kiloba cha magimbi katika soko hilo kiliuzwa kwa sh.100,000, mihogo sh.45,000 rejareja 1,000,  viazi vitamu sh.100,000  rejareja 1500na ndizi mkungu sh.16,000 hadi 19,000 na rejareja 1,000.
Naye mteja wa ndizi katika soko hilo, Asia Mohamed  alisema serikali iangalie upandishaji holela wa vyakula katika kipindi hiki cha mwezi wa Ramadhani.
“Tunaiomba serikali iangalie kwa makini suala la upandishaji holela wa vyakula kwani tunapata shida sisi tuliofunga , huku ni kutufanyia makusudi ili wafanyabiashara wajipatie fedha nyingi kipindi hiki,” alisema.
                                     


TWANGA PEPETA WAVURUGANA



BAADHI ya wanamuziki wa Bendi ya The African band ‘Twanga pepeta’ wametishia kuihama bandi hiyo kutokana na kile walichokiita kunyanyaswa na viongozi wa bendi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti kwa sharti la kutotajwa majina yao, wanamuziki hao walisema kumekuwepo na manyanyaso katika bendi hiyo kwa kuwabagua katika kuwalipa mishahara.
“Tumechoshwa na ubaguzi huu maana kwenye kufanya kazi hatubaguliwi lakini wakati wa kulipwa fedha zetu zinakaa miezi miwili wakati kuna wenzetu wanalipwa mapema,” alisema mmoja wa wanamuziki hao.
Mwanamuziki mwingine alisema wamekuwa wakitengwa hasa kipindi cha malipo kwa kuonekana wengine ni bora kuliko wao.
“Kama familia tunazo wote na kila mtu ana majukumu sasa kwa nini wengine walipwe kwa wakati? Kila mmoja amekuja kutafuta pesa,” alisema.  

HATIMAYE ALLY CHOKI AOA



MKONGWEwa muziki wa dansi na mwimbaji wa bendi ya The African star, Ally Choki  ‘Kamarade’ amepata jiko baada ya kuishi mpweke kutokana na kufiwa na mkewe marehemu Mama Shuu.
Akizungumza kwa sharti la kutoandikwa jina Gazetini, mmoja wa karibu na Staa huyo alisema Ally Choki aliamua kufunga ndoa na mwanamke aliyezaa naye.
“Choki amefunga ndoa na mwanamke aliyekuwa amezaa naye hivi karibuni ili apate mtu wakumpikia futari,”kilisema chanzo hicho.

Jumanne, 16 Juni 2015

JAJI MUTUNGI: MCHAKATO WA KUTAFUTA MGOMBEA URAISI KWA SASA HAUNIHUSU



MSAJILI wa Vyama vya siasa nchini Jaji Francis Mutungi amesema  mchakato wa kutafuta wagombea  urais unaoendelea ndani  ya vyama hauhusiani  na ofisi yake na kuwataka wananchi kuacha demokrasia ifanye kazi  ndani ya vyama husika.
Akizungumza jijini jana Jaji Mutungi alisema jamii inapaswa iache kila chama ifanye kazi kwakukuza demokrasia   katika mchakato huo wa hatua za awali na endapo kuna mtu ataenda kinyume na taratibu sheria itaweza kumbana badae kupitia pingamizi za wananchi.
“Watu wengi walikuwa wakifikiri ofisi ipo kimya  na hili suala si kweli,huwa tunawasiliana na wadau husika kwa mujibu wa taratibu   hatua ya kwenda kwenye public(umma) ni ya mwisho,kama chama kimesajiliwa tuache demokrasia ifanye kazi yake  mchakato wa ndani ya chama huwa hatuna mamlaka nao,”alisema Jaji Mutungi.
Alisema ni mapema sana kutoa tathimini ya utekelezaji wa sheria ya gharama za uchaguzi kwakuwa kwa sasa ofisi hiyo kazi yao ni kuangalia tu na si vinginevyo   muda ukifika watachukua hatua kwa mujibu wa sheria kwakuzingatia malalamiko ya wahusika.
Alisema sheria ya gharama za uchaguzi madhumuni ina lengo la kudhibiti matumizi katika chaguzi na vitendo vinavyokatazwa  na sheria ya nchi.
Alisema wananchi na wadau wa siasa wanapaswa kuzingatia sheria ya gharama za uchaguzi na kanuni zake za kikomo cha gharama ili kuondoa usumbufu  badae.
“Natoa tahadhali na angalizo kwa vyama vya siasa na wanasiasa wasipuuzie sheria  na kanuni hizi zitawaathiri nje na ndani ya chama,wanaweza wakahatarisha uteuzi wao na chama kisipofuatilia na kupitisha mgombea atawekewa pingamizi  harakati zote wanazozifanya zitakuwa hazina maana,”alisema Jaji Mutungi.
Akizungumzia kuhusu vikundi vya ulinzi na usalama vya ndani ya vyama Jaji Mutungi alisema sheria ya vyama vya siasa inapiga marufuku vyama kuanzisha vikundi ambayo vinavyofanya kazi sawa na jeshi na polisi.
Alisema kwa mujibu wa sheria ya vyama vya siasa vikundi vya wanachama vilikuwa na jukumu la kuangalia usalama wa mali za chama  bila kupewa mafunzo ya kijeshi na vyeo kama wanavyofanya sasa.
“Kwa bahati mbaya kutokana na sababu ambazo zinafahamika kwa vyama vya siasa,vyama hivi vimebadili mfumo,jina,uendeshaji na muelekeo wa vikundi hivi na kuwa na mfumo wa kijeshi .
Baadhi ya vyama vikaviita vikosi vya ulinzi na usalama wa vyama(guard) kuanzisha mafunzo maalum ya kujilinda,ukakamavu  na kupambana na hata kuwekwa vyeo kama vya jeshi,jambo hili ni ukiukwaji wa sheria ya nchi hivyo navitaka vyama vilivyofanya hivyo kuvivunja vikundi mara moja,”alisema Jaji Mutungi.
Alisema katiba ya chama chochote yenye kipengele cha kuwa na jeshi ndani ni batili  na endapo wanataka mabadiliko ya wanapaswa kufuata taratibu  ikiwemo kushawishi kubadilika kwa sheria hiyo.