Jumamosi, 31 Desemba 2016

MANJI AMTIKISA MWINYI

MGOGORO wa ardhi unaohusisha vijiji vinne vya Wilaya ya Mkuranga umechukua sura mpya baada ya Mkuu wa Wilaya hiyo, Filberto Sanga  kuwataka wakazi wa vijiji hivyo kukaa vikao vya kutayarisha mihutasari kumwomba Rais kufuta hati ya shamba ambalo limekuwa likitumiwa na wananchi kwa muda mrefu.
Mgogoro huo wa eneo la ekari 2472 unahusisha vijiji vinne vya kata mbili ya Tambani na Mipeko vyenye wakazi takribani 45,000 wakiwamo Rais Mstaafu Ali Hassani Mwinyi, Salim Ahmed Salim, Jaji Joseph Warioba, Jaji Hamis Msumi, Rashidi Kawawa wakihusishwa kuvamia eneo la Kareem Manji na Entias Rajuani.


Sanga aliyasema hayo katika mkutano wa hadhara kati ya wananchi na kamati ya usalama ya wilaya hiyo uliokuwa na lengo la kujadili shamba hilo linaloonekana kutishia usalama wa raia pamoja na mali zao.
Alisema viongozi wa vijiji hivyo wanapaswa kuhakikisha shughuli zote za upimaji ardhi katika vijiji hivyo vilivyodaiwa kumilikiwa na wamiliki hao zinasitishwa mpaka pale taratibu mbalimbali zitakapokamilishwa.

Alisema viongozi wa vijiji hivyo wanapaswa kuhakikisha hakuna mtu yeyote anayeweza kufanya maamuzi ya aina yoyote katika vijiji hivyo pasipo kupata ruhusa na kibali kutoka katika ofisi za Serikali.
 “Anzeni vikao kujadili suala hili na kuandika muhtasari kwa ngazi za juu kuomba kufutwa umiliki wa shamba hili,” alisema Sanga.
Sanga aliwahakikishia wananchi wa eneo hilo kuwa wako katika mikono salama kuwa hakuna atakayewaondoa katika eneo hilo bila kufuata sheria.

“Mimi mkuu wa wilaya sina ardhi ya kuwaweka watu 45,000 wanaoondolewa hapa hivyo wakija waambieni waanzie kwangu… kwani kuwagusa wananchi bila kupitia viongozi huo ni uhuni,” ali
sema.
Aliwatahadhalisha wananchi kutouza holela ardhi jambo ambao husababisha migogoro kuwa mingi.
“Acheni kuuza ardhi, niwaombe wenyeviti wasaidieni wananchi wasiuze ardhi, na kama mtu anauza eneo lake uuzaji huo ufanyike hadharani kwa yeye na mnunuzi kusimama mbele ya wananchi ili mgogoro ukitokea wao ndio wawe wa kwanza kusuluhisha,” alisema Sanga.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo,Mhandisi Ally Munde

Naye mbunge wa Jimbo la Mkuranga, Abdallah Ulega amemuomba Rais Dk. John Magufuli kufuta hatimiliki ya shamba hilo baada ya wawekezaji hao kushindwa kuliendeleza kwa zaidi ya miaka 50 na badala yake wapewe wananchi.
 Alisema shamba hilo lilitelekezwa kwa kipindi kirefu na wawekezaji hao, hali iliyopelekea wakazi wa kata ya Tambani pamoja na Mipeko kuyaendeleza kwa kufanya ujenzi na shughuli mbalimbali za maendeleo.
Ulega alisema Wakazi wa maeneo hayo waliweza kutafuta hati miliki ya maeneo waliyokuwa wanamiliki kwa kipindi chote na kushangazwa na kitendo cha wamiliki hao kuwataka kutoka katika maeneo yao kwa madai kuwa wamevamia eneo hilo.
Alisema wananchi wa vijiji vya Mlamleni, Luzando, Mwanambaya pamoja na Mipeko wamekuwa katika hali ya taharuki toka walipopewa notisi ya siku 21 ya kuwataka waondoke katika maeneo hayo ambayo wameyaendeleza kwa shughuli mbalimbali za kimaendeleo.
"Mi najua Rais wetu ni msikivu na anaweza kuzifanyia kazi kero za wananchi kwa wakati, na kero hii naamini atatilia mkazo kwa sababu wameshindwa kufanya shughuli za maendeleo kwa sasa kwa sababu ya watu wawili ,” alisema Ulega.
 Hata hivyo Ulega alimueleza Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga kumuagiza Ofisa Ardhi Mteule
 alimweleza Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kutoruhusu kampuni ya 'Ardhi Plan' kupima maeneo ya wilaya hiyo kwani kama ataruhusu kampuni hiyo kufanya upimaji watapelekea kutokea kwa vurugu ambazo zinaweza kusababisha hali ya amani na utulivu kutokuwepo katika wilaya hiyo.
Naye Mbunge wa jimbo la Mkuranga Abdallah Ulega ambaye pia ni muhanga alisema walikubwa na taharuki baada ya kupokea notisi ya siku 21 ikiwataka kuondoka katika eneo hilo.
“Tutafuata taratibu na sheria kufikisha kilio chetu kwa rais kumwomba alifutite shamba hilo kwa kuwa alishindwa kuliendeleza kwa muda wa zaidi ya miaka 50,” alisema Ulega.
Alimwomba DC kumwagiza Ofisa Ardhi mteule kumpa mmiliki huyo notisi ya siku 90 ya kusudio la kulifuta shamba hilo.
“Hakuna shamba hapa, ninaona nyumba za watu tu, hivi mimi DC mstaafu nitapata wapi tena fedha za kununua kiwanja,” alisema Ulega.
Akisimulia historia ya shamba hilo la Luzando, Diwani wa kata ya Tambani, Ally Mtamilwa alisema shamba hilo lenye hati namba 1281 lilimilikiwa na kampuni ya Mzungu iliyoitwa Seneda aliyekuwa akilima mkonge kabla ya kuhamishiwa kwa Akibaru February,1952.
“Mwaka 1978 Waziri Mkuu wa wakati huo hayati, Edward Sokoine alitangaza vijiji vya nguvu kazi vikiwamo Mwanadilatu, Gezaulole,Tegeta na katika shamba hilo ili walima kipindi hicho Akibaru aliondoka muda mrefu,” alisema Mtamilwa.
Alisema baada ya watu hao kupelekwa katika mashamba ya nguvu kazi waliendelea kuishi hapo kabla ya wanaodaiwa kuwa ni wajukuu wa Akibaru ambao ni Manji na Rajuani kufika katika eneo hilo kwa madai ya kutaka kuliendeleza wakiwa na hati ya mwaka 1952.
“Baada ya kukuta wananchi wakiendelea na kilimo waliridhia kutoa ekari 1472 kwa wananchi na wao kubakiwa na ekari 1,000 ambapo mwaka 1990 walifanya tathmini ya kuwaondoa wananchi waliokuwa ndani ya ekari walizobakiza na waliondoka bila kuwalipa,” alisema Mtamilwa.
Mtamilwa alisema Manji na mwenzake walituma kampuni ya upimaji wa ardhi iitwayo Ardhi Plan kupima viwanja katika eneo hilo.
“Waliwataka wenye maeneo ambayo hayajajengwa kulipwa kila ekari shilingi milioni moja na waliojenga kupimiwa viwanja na kulipa gharama za upimaji,” alisema Mtamilwa.
Aliongeza kuwa baada ya wananchi kutokuafiki suala hilo ndipo Manji na mwenzake kupitia mwanasheria wao waliandika notisi ya siku 21 kuwataka wakazi hao kuondoka kabla ya Disemba 19, 2016.
mwisho




Jumatatu, 19 Desemba 2016

JELA MIAKA MINNE KWA KUNG'ATA NA KUMEZA SIKIO LA CHACHA

MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala imemhukumu kwenda jela miaka minne, Chacha  Nyanchini baada ya kupatikana na hatia ya kumng’ata sikio na kulimeza ndugu yake ambaye ni Chacha Kiong’otu maarufu kama Chacha.
Hukumu hiyo ilitolewa juzi mahakamani hapo na Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Adelf Sachore baada ya kujiridhisha na hoja za upande wa mashtaka ambao ulikuwa na mashahidi watano waliotoa ushahidi pasi na kuacha shaka.
“Ninakuhukumu kutumikia kifungo cha miaka minne baada ya kupatikana na hatia ya kumng’ata sikio la kutosha na kukimeza kipande cha sikio cha mlalamikaji huku ukijua fika kuwa kufanya hivyo ni kosa kwa mujibu wa taratibu za nchi,” alisema Sachore.
Awali kabla ya hukumu hiyo kutolewa wakili wa Serikali, Chesence Gavyole alidai kuwa hakukuwa nakumbu kumbu za mashtaka ya nyuma dhidi ya mshtakiwa na hivyo kuiomba mahakama kutoa adhabu kali ili iwe fundisho kwa wote wenye tabia kama hizo za kung’ata wenzao.
Katika utetezi wake juu ya kwanini mahakama isimpatie adhabu kali, Nyanchini alidsai kuwa anafamilia inayomtegemea na kwamba hakukusudia kufanya hivyo, hivyo mahakama imsamehe kwa kuwa lilikuwa ni kosa lake la kwanza utetezi ambao ulitupiliwa mbali.
Kwa mujibu wa hati ya mashtaka ilidaiwa kuwa Februari 12, mwaka huu katika eneo la Kivule Majohe ndani ya Wilaya ya Ilala Dar es Salaam alimng’ata na meno sikio la kushoto la mlalamikaji na kukimeza kipande hicho kwa kile kilichodaiw akuwa kuwa ni ugomvi wa kifamilia.

Mwisho 

Alhamisi, 15 Desemba 2016

Platinum Credit kudhamini uchunguzi saratani ya shingo ya kizazi

KAMPUNI ya Platinum Credit Ltd kwa kushirikiana na Hospitali ya mkoa ya Mwananyamala watatoa bure huduma za uchunguzi wa saratani ya shingo ya kizazi kwa wanawake jijini Dar es Salaam.
 Akizungumza na waandishi wa habari jana Meneja Mauzo wa kampuni hiyo, Lufunyo Gideon alisema wameamua kufadhili uchunguzi huo ikiwa ni zawadi ya sikukuu ya Chrismas na kurudisha kile walichokipata kwa jamii.
Alisema uchunguzi huo utafanyika katika hospitali ya Mwananyamala iliyopo Kinondoni jijini Dar es Salaam kuanzia kesho hadi Disemba 21, mwaka huu.
“Tunawaomba wanawake wajitokeze kwa wingi katika kufanyiwa uchunguzi ili waweze kutambua afya zao mapema na kupata ushauri,” alisema Gideon.
Naye Mganga mfawidhi wa Hospitali ya Mwananyamala Dk.Daniel Nkungu alisema ni fursa kwa wanawake kujua afya zao ili kama wana ugonjwa huo wapate matibabu mapema.
“Tatizo lililopo kwa sasa ni watu kuchelewa kugundua dalili za awali za ugonjwa huo hivyo kugundulika ukiwa katika hatua mbaya ambayo mara kadhaa umekisababisha vifo,” alisema Dk.Nkungu.
Alisema wahudumu wa hospitali hiyo wamejipanga vizuri kuendesha uchunguzi huo hivyo wasiogope kwa kudhani kutakuwapo na foleni kubwa.

“Niwaombe wanawake wajitokeze kwa wingi kupima kwa kuwa tumejipanga vizuri katika kuwapokea na kuwafanyia uchunguzi kwa haraka,” alisema Dk.Nkungu.

Jumatano, 7 Desemba 2016

kampuni yadai kuidai TPA Bil.2

KAMPUNI ya Baga Investment imeshindwa kulipa kwa wakati posho za baadhi ya wafanyakazi wake kwa madai ya kuidai Mamlaka ya Bandari Tanzani(TPA) shilingi bilioni 2.

Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni hiyo, Jumbe Moshi, aliyasema hayo jana baada ya kuwapo kwa malalamiko ya baadhi ya wafanyakazi wa kampuni hiyo ambao wanalipwa kwa siku kudai kutolipwa posho zao kwa siku 23.
Alisema ni zaidi ya miezi mitatu sasa TPA imeshindwa kuwalipa fedha hizo hivyo kushindwa kulipa madeni yanayowakabili yakiwamo ya Benki.

“Kuchelewa kulipwa kwa wafanyakazi wetu kunatokana na TPA kushindwa kuilipa kampuni kwa miezi mitatu jambo ambalo linarudisha nyuma utendaji wa kampuni.

 “Hali hii imetuweka katika wakati mgumu kutokana na kampuni kudaiwa na baadhi ya Benki hali inayofanya tushindwe kulipa na kujiendesha,” alisema Moshi.
 Moshi alisema kuwa kampuni hiyo iliingia mkataba na TPA wa kufanya kazi za ufundi wa kutengeneza maboti, magari na udereva wa folk ambapo kampuni hiyo ilianza kazi hizo mwaka 2012.
 “Tunakutana nao mara kwa mara na wanatuomba radhi kwa kututaka tuvute subira mambo yakikaa sawa watatulipa,”alisema Moshi.

Akizungumzia malalamiko ya wafanyakazi hao, Moshi alisema kampuni hiyo imejitahidi kulipa posho za wiki iliyopita lakini juhudi zinaendelea kufuatilia fedha wanazozidai TPA ili waweze kuwalipa fedha zao zote.

Aidha Moshi alisema wafanyakazi hao licha ya kulipwa kwa siku lakini kutokana na makubaliano yao kila mmoja anapofanikiwa kuingia kazini lazima anapelekewa makato yake NSSF.

Awali baadhi ya wafanyakazi wa Kampuni hiyo ya Baga Investment, walidai kuwa hawajalipwa posho hizo kwa siku 23 sasa.

Mmoja wa wafanyakazi hao ambaye hakutaka kuandikwa gazetini alisema kila walipouliza walijibiwa kwamba chimbuko la kuchelewa huko kumesababishwa na TPA  ambayo haijailipa kampuni hiyo kwa zaidi ya miezi mitatu.

Akizungumzia malalamiko hayo, Msemaji wa Bandari Janet Ruzangi alisema madai hayo hayana ukweli kwa sababu kampuni hiyo inalipwa kwa wiki.
“Sijui mkataba wao na TPA unasemaje lakini mara nyingi malipo yao yanakuwa kwa wiki au mwezi kwa sababu Baga Investment mpaka wameingia mkataba na kuendesha shughuli hiyo inamaana walikuwa wanazo fedha za kutosha na siyo mpaka walipwe,” alisema Ruzangi.



Jumanne, 6 Desemba 2016

ACT WAFUKUA MAKABURI ATCL



CHAMA cha ACT-Wazalendo kimesema Makaburu walimrubuni Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi wakati huo, William Kusila, akasaini mkataba kati ya mikataba ya Alliance Air kwenye karatasi ikiwa na nembo ya wizara bila ya maandishi yoyote na kuwapatia makaburu waende wakajaze maelezo wanayoyataka nchini kwao jambo lililochangia kuitesa Air Tanzania hadi leo. 

hayo yalisema jana na Mwenyekiti wa Chama hicho, Anna MghwiraAnna alipozungumza na waandishi wa habari ambapo alisema miaka ya 1990 viongozi wa Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi kupitia kitendo cha usafiri wa anga waliuza njia(Routes) za ATCL kwa mashirika mengine ya ndege na kuilazimisha ATCL kuingia katika mikataba mibovu ya ushirikiano  na kulifilisi shilika hilo.
“Kwa ujanja kampuni ya Swissport ilianzishwa ikiwa chini ya mkurugenzi wake Esther Maro ambaye alikuwa ni mdogo wake Anna Mkapa, na kulinyang’anya shirika majukumu yake huku Gulf Air, Emirates na Kenya Airways zikiongezewa njia na wakawa waendeshaji wa njia kama mashirika ya Taifa la Tanzania,” alisema Anna.   
Alisema katika awamu ya tatu na nne ATC ilinyang’anywa huduma za chini uwanjani na kulazimishwa kuingia ubia na South African Airways(SAA) na Makaburu hao kuilazimisha menejimenti na bodi ya ATC kupunguza marubani15 na wahandisi 30 kwa kuwadanganya kuuza ndege za kizamani.
“Ndege zilizouzwa aina ya B737-200 zilikuwa zinaruka vizuri kwa safari za ndani na nje zilifika Ulaya, Marekani na Afrka kusini, ambazo zilituwa na makampuni mengi kwa ahadi ya kutuletea za kisasa zenye uwezo wa kusafiri umbali mrefu,” alisema Anna.

aidha kimeishauri serikali kulirudishia Shirika la Ndege la Taifa(ATCL) mamlaka ya kumiliki huduma zote za chini(Ground handling) za uendeshaji wa viwanja vya ndege.
Pia wameiomba serikiali kuunda kitengo cha uwezeshaji ambacho kitahudumia shughuli zote zinazofanyika katika viwanja vya ndege nchini ili kuimarisha usalama wa nchi.
 alisema huduma hizo ni pamoja na huduma kwa abiria, kuhudumia mizigo yote ya Ndege, huduma za vyakula na kambi ndani ya ndege na ukatishaji wa tiketi.
Alisema huduma hizo ni moja ya vitega uchumi muhimu katika mashirika ya ndege ya nchi, Duniani kote kwa kuwa biashara ya ndege haitegemei kuwa na ndege pekee hivyo kutaka maandalizi yaanze mapema ili zikiwasili mfumo wa uzalishaji uko vizuri.
“Kwa kutoa huduma hizi kwa umakini na kuvimilikisha viwanja kwa wananchi wazalendo ambao watakuwa waajiriwa wake, shirika litaweza kuzalisha fedha nyingi na kutoa ajira kwa watanzania,” alisema Anna.
Alisema kwa muda mrefu sasa Tanzania imekwenda kinyume na utaratibu huo jambo ambalo ni kuinyakulia ATCL raslimali zake na hivyo kuinyima mapato.
Alisema ubinafsishaji wa raslimali hizo haukufanyika kwa lengo la kuimarisha usimamizi bali ulichangiwa na tabia ya rushwa ya kupata asilimia kumi ya faida kwa viongozi walioongoza na kulididimiza taifa.
“Uendeshaji wa mifumo ya compyuta,mfumo wa usalama wa viwanja, utunzaji wa mizigo, utunzaji wa abiria, kitengo cha uhandisi na huduma ya kuuza mafuta ya ndege viwe chini ya shirika kwa ajili ya usalama wa nchi na kuzalisha ajira,  kwani ni rahisi kwa wageni kurubuniwa” alisema Anna.
 
     

Jumapili, 4 Desemba 2016

QUALITY WAISOMA


KAMPUNI ya Quality Group inayomilikiwa na mfanyabiashara Yusuf Manji imeondolewa katika jengo iliyokuwa ikilikalia lililoko kiwanja namba 189/2 barabara ya Nyerere, jijini Dar es Salaam kutokana na deni la malimbikizo ya ya pango la shilingi bilioni 13.
Kampuni hiyo inadaiwa kiasi hicho cha fedha kutokana na kulimbikiza deni hilo kwa miaka mingi tangu ipangishwe na mmiliki wa jengo hilo ambaye ni Mfuko wa Pensheni wa PSPF.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Meneja wa Operesheni wa kampuni ya Udalali ya Yono ambao ndio walipewa zabuni ya kuiondoa kampuni hiyo, Atukuzwe Muhugo alisema kazi hiyo imefanikiwa baada ya kutoa notisi ya masaa 24 kuitaka iondoke.
Alisema notisi hiyo iliisha alfajiri ya jana ndipo walipofika kuiondoa kwa nguvu lakini wafanyakazi walitii sheria na kuanza kutoa mali zao.
“Wafanyakazi wa Quality Group hawakuwa wajeuli wametii amri bila shuruti jambo lililoturahisishia kazi yetu,” alisema Atukuzwe.
Alisem jengo hilo litakuwa chini ya Yono mpaka hapo litakapokabidhiwa kwa PSPF.
Aliyataja ofisi zilizoondolewa kuwa ni Chief Exercutive officer of Quality Group Company LTD, Gaming Management Ltd, Q Consult Ltd, Quality Logistics Company Ltd na International Transit Investment Ltd .
Mmoja wa mahusika katika kampuni hiyo ambaye hakutaka kutaja jina lake alipotakiwa kuzungumzia tukio hilo alisema hajajiandaa kuongea na wanahabari na hivyo kuwaomba wafike leo saa nane mchana ndipo ataongea.
“I don’t have suit, come tomorrow I will be ready to talk to you, how could I talk to you without wearing suit? Come tomorrow after lunch on 2  (siwezi kuzungumza bila kuvaa suti hivyo nawaomba mje kesho saa nane mchana ),” alisema.
Ilishuhudiwa magari aina ya Isuzu yenye namba za usajili T385 DAB na T620 DCC yakipakia vitu na kupeleka sehemu ambayo haikujulikana mara moja.
Uamuzi wa kuindoa Quality Group katika jengo hilo umetokana na kushindwa katika kesi namba 33 ya mwaka 2009 iliyofungua kampuni hiyo  katika mahakama kuu, Divisheni ya ardhi ikipinga kuondolewa.
Kesi hiyo ilimalizika Novemba 24, mwaka huu kwa mahakama kumpa haki mmiliki wa jengo hilo PSPF kutafuta dalali wa kumwondoa Quality Group.

Jaji aliyetoa hukumu hiyo aliamuru kuondolewa kwa Kampuni hiyo  na kuiacha PSPF kama mmiliki wa jengo hilo na ndipo Yono walipopewa zabuni ya kwenda kumwondoa.

Alhamisi, 1 Desemba 2016

ULEGA AAHIDI KUBORESHA HUDUMA ZA AFYA

MBUNGE wa Mkuranga Abdallah Ulega(CCM), ameahidi kushughulikia malalamiko ya kukosekana kwa hudumu za afya katika Zahanati ya Mkamba.
Ulega aliahidi hayo wakati akizungumza na Halmashauri Kuu ya Kata ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwashukuru kwa kukisaidia chama hicho kupata ushindi.
Alisema  serikali ya CCM ni sikivu anahakika wahudumu watapatikana kwa ajili ya kuboresha huduma hiyo.
Alisema, baada ya kupokea taarifa hiyo anahakikisha anaifikisha katika sehemu husika kwa ajili ya kufanyiwa utekelezaji.
"Nitahakikisha ujumbe unawafikia wizarani kwa ajili kupatiwa wahudumu hao ambao watakuja kuondoa kero hii inayotukabili katika kata hii sitakubali kuona CCM inatiwa masingi kutokana na kushindwa kuwahudumia wananchi,"alisema Ulega.
Aidha Ulega aliahidi kuanza mara moja ujenzi wa barabara ya kutoka Kimanzichana kwenda katika kata hiyo ili kuondoa adha ya usafiri inayowakabili.
"Wazee wangu Mimi na diwani wenu tutafanya kila linalowezekana kutengeneza japo kwa dharura barabara hii ili iweze kutumika tukiwa tunasubiri fungi la serikali," alisema Ulega.
Kwa upande wake mkazi wa kata hiyo, Mikidadi Misomba alimweleza Ulega kuwa akiweza kutatua matatizo manne yanayowàkabili, wao kama wazee wa CCM watatembea kifua mbele.
"Mahitaji yetu ni manne ukitutimizia utakuwa umetuondolea aibu sisi wazee wa CCM ambayo ni kutuboreshea huduma za afya, barabara,maji na kutuondolea wavamizi wenye mifugo ambao wamekuwa wakituharibia mazao na kusababisha njaa," alisema Misomba.

nicol wapata hasara ya bil.10


KAMPUNI ya uwekezaji ya wazawa(NICOL), imeanza uchunguzi wa hasara ya shilingi bilioni 10 iliyopata baada ya kufanya uwekezaji mbaya katika kampuni mbili tofauti.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa NICOL, Gideon Kaunda alisema uchunguzi huo utafanyika ndani ya wiki mbili na baada ya ripoti kukabidhiwa watawafungulia kesi mahakamani wote waliosababisha hasara hiyo.
Alisema hadi kufikia Disemba 31, 2009, kampuni hiyo ilipata hasara hiyo kutokana na kuwekeza katika kampuni ambazo baadaye zilifilisiwa na benki zilizokuwa zikizidai.
“NICOL iliwekeza Dola za Marekani Milioni mbili(sawa na shilingi bilioni nne) katika kiwanda cha kutengeneza dawa kilichopo Moshi, mkoani Kilimanjaro ambacho kilikuwa kimekopa katika benki ya Barclays na baada ya kushindwa kulipa deni hilo benki ilikitaifisha na kusababisha fedha hizi kupotea,” alisema Kaunda.
Alisema katika uwekezaji mwingine NICOL iliwekeza shilingi bilioni tatu katika kiwanda cha samaki kilichopo Mwanza na baadaye kukiongezea shilingi bilioni tatu ambacho nacho kilikopa fedha katika Benki ya Maendeleo ya Afrika(ADB).
“Baada ya uwekezaji wa mwaka mmoja kilishindwa kulipa deni hilo lililosababisha kufilisiwa na benki hiyo hivyo kupoteza fedha hizo,” alisema Kaunda.
Alisema pia wamebaini kuwa kutokana na uzembe ulifanyika katika kipindi cha uongozi wa Mwenyekiti wa zamani, Felix Mosha umesababisha kampuni tanzu ya Tanzania Meat Company ltd na ile ya Mwanza kufanya ubadhilifu.
“Mbali na kuwapo kwa matumizi mabaya ya fedha pia kodi za serikali na michango ya watumishi katika mifuko ya hifadhi za jamii haikuwa ikipelekwa hivyo kuongeza madeni,” alisema Kaunda.
Alisema katika uchunguzi huo pia wataangalia upya mikataba ya kampuni za nje zinazonunua nyama iliyoingiwa na TMC kutokana na kuwa na mapungufu mengi.
Aidha Kaunda alisema mapema mwakani wataanza kuwekeza tena katika soko la hisa baada ya kumalizika kwa migogoro ya uongozi iliyokuwapo awali.
mwisho