Jumapili, 15 Mei 2016

WAJIFUNGULIA KWENYE MABOTI KWA KUKOSA VITUO VYA AFYA



WANANCHI wa Vijiji vya Koma na Kwale,  Wilayani Mkuranga mkoani Pwani, wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa vituo vya afya, hali inayosababisha kupoteza maisha na wanawake kujifungilia kwenye boti wakati wakifuata huduma hiyo Wilayani.

Wananchi hao walitoa malalamiko yao mbele ya Mbunge wa Jimbo la Mkuranga, Abdallah Ulega,  juzi alipofanya ziara ya siku moja ya kutembelea visiwa hivyo  kuwashukuru wananchi kwa kumchangua kuwa mwakilishi wao pamoja na kukagua miradi ya maendeleo.

Mmoja wa wanakijiji hao, Maimuna Nyakonda, alisema  kuwa wanawake wamekuwa wakipata madhara wakati wakisubiri usafiri wa boti kuwavusha na kuwapeleka Wilayani Mkuranga kwa matibabu lakini kwa bahati mbaya wamekuwa wakizalia njiani na wengine kuzalishwa na wakunga kutokana na hali ya hewa.

"Ukosefu wa zahanati katika Vijiji hivi ambavyo viko kisiwani, umesababisha sisi wanawake kudhalilika sana, tunajifungulia njiani huku mabaharia wakishuhudia pia wakati mwingine wenzetu wanapoteza maisha, hili jambo linatusononesha sana, " alisema Maimuna.

Naye Halima Said, mkazi wa kijiji cha Koma, alisema hali hiyo imesababisha wanawake wa visiwa hivyo kuendelea kutegemea huduma za wakunga ambao hawana ujuzi na kusababisha madhara kwa wanaojufungua.

"Huku tunatumia njia mbili tu kuhamia Wilayani wakati mimba inapofikia miezi nane au kama huna ndugu huko ubaki hapa, kama Mungu akisaidia kukawa na hali ya hewa nzuri bahari haijachafuka,  unaweza kufika Wilayani salama,” alisema.
Alisema kama ikishindikana wanalazimika kwenda kwa mkunga ambaye hata hivyo hawana ujuzi wa kumsafisha mama aliyejifungua vizuri.
Akizungumza tatizo hilo, Ulega alisema, tayari ameanza kujenga Zahanati katika kijiji cha Koma ambayo inatarajia kukamilika mwaka huu na katika kijiji cha Kwale ameagiza uongozi wa kijiji na halmashauri kuanzisha ujenzi ili aweze kuendeleza.

"Natambua shida mnazopata mama zangu, naahidi mwaka huu hautaisha bila zahanati hii kukamilika lakini pia naandaa utaratibu wa kujenga nyumba ya mganga,  kununua thamani zote za ndani ili mganga aje tu na nguo, awape huduma wananchi wangu wa Koma, "alisema Ulega. 
Alifafanua kuwa, katika kipindi chake cha miaka mitano ya uongozi anatarajia kujenga zahanati  na vituo vya afya 30 ili wananchi na wapate huduma ya afya iliyo bora.
 MWISHO

Jumapili, 1 Mei 2016

watumishi wa serikali mkoa wa Dar kujengewa nyumba



WAFANYAKAZI wa serikali wa mkoa wa Dar es Salaam wameahidiwa kujengewa nyumba katika viwanja vyao ili kuondokana na kero za kodi za nyumba.
Akizungumza katika maadhimisho ya sikukuu ya wafanyakazi ilivyofanyika kimkoa jijini Dar es Salaam Mkuu wa Mkoa wa huo, Paul Makonda alisema wafanyakazi wamekuwa wakipata taabu nyingi kutokana na mishahara kutokidhi mahitaji ya kodi za nyumba na gharama za maisha.
Alisema mishahara wanayopata haiwezi kutosha kuhimili mazingira ya maisha ya jiji la Dar es Salaam.
“Sisi kama serikali ya mkoa tumekaa na kufikiri kuona namna ya kutafuta watu watakaowajengea nyumba ndani ya miezi sita katika viwanja vyenu nanyi mtalipa taratibu,” alisema Makonda.
Alisema tayari wamenza kutengeneza baadhi ya ramani ambazo wafanyakazi hao watachagua wanazozitaka.
“Mtalipa taratibu kwa kuwa nyinyi ni watumishi wa umma na mimi kama mkuu wa mkoa nitawadhamini,” alisema Makonda.
Aliongeza kuwa katika hatua za uboreshaji wa mazingira ya kufanyia kazi wameanza na walimu ambao ni kundi kubwa kwa kuwawezesha kusafiri bure.
“Lengo langu halikuwa kuishia katika usafiri wa daladala bali utasaidia hata katika mabasi yaendayo kasi japo nilisikitika sana kusikia baadhi ya viongozi wenu kutoa kauli ya kukataa eti kwa sababu wanadai wanamalimbiko na nyongeza ya mishahara.
Leo umenikuta mwenge unaniomba nauli ya kwenda posta kwa daladala mimi nakwambia nina  gari unaanza kutoa sababu za kuwa huna chakula,” alisema Makonda.
Aidha alisema katika kuhakikisha jiji la Dar es Salaam wanatarajia kuachana na matumizi ya mifuko ya plastiki maarufu kama Rambo.
“Niwaombe viwanda wanaotengeneza mifuko hiyo watubadilishie mifuko hii wa ndani ya siku 90,” alisema Makonda.  
Awali akisoma Risala kwa mgeni Rasmi, Mratibu wa maadhimisho hayo, Elias Chizingwa alisema wafanyakazi wa mkoa huo wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwamo mishahara duni isiyokidhi mahitaji hasa katika jiji la Dar es Salaam, wafanyakazi kukatwa kodi mara tatu, baadhi ya waajiri kuchelewesha kupeleka michango katika mifuko ya hifadhi za jamii.
“Changamoto nyingine ni mazingira magumu ya kufundishia walimu, baadhi ya waajiri kutokuvitambua vyama vya wafanyakazi na baadhi ya makampuni ya wawekezaji wa nje kuwanyanyasa wafanyakazi wazalendokwa kuwafanyisha kazi kwa masaa zaidi 18,” alisema  Chizingwa.
mwisho

Jumatano, 3 Februari 2016

TAHARUKI KIVUKO CHAPOTEZA UELEKEO

TAHARUKI imetanda katika maeneo ya Kivuko cha Feri, jijini Dar es Salaam baada ya kudaiwa kivuko cha MV Magogoni kukwama najini na kupoteza uelekeo kutokana na upepo mkali uliokuwa ukivuma jana asubuhi katika Bahari ya Hindi.
FICHUA ilifika maeneo hayo na kukuta baadhi ya wananchi wakielezea tukio hilo ambao walidai kivuko hicho kilipoteza mwelekeo na kusababisha taharuki kwa wananchi wanaotumia usafiri huo.
“ Kuna kivuko leo kilikuwa kimepakia abiria kikasombwa na upepo na kupelekwa umbali mrefu hadi walipopata msaada wa kuvutwa baada ya masaa matatu kuanzia saa moja hadi saatatu asubuhi,” alisema mmoja wa shuhuda aliyejitambulisha kwa jina la Asia Rajab.
Alisema kivuko hicho kilikwama kwa muda wa masaa matatu  hivyo kuleta usumbufu mkubwa kwa wasafiri wanaotumia usafiri huo.
Alisema hali hiyo imewafanya abiria kuogopa kukitumia kivuko hicho kwa hofu ya kuzama majini.
 
Hata hivyo Ofisa Habari wa TEMESA Theresia Mwami alikiri kupata taarifa hizo na kudai kuwa  wanazifanyia kazi na watatoa taarifa itakapokuwa tayari.
Wakati huohuo, Mamlaka ya Hali ya Hewa (Tma), jana imetoa tahadhari wananchi wa Ukanda wa Pwani kwakuwa kutakuwa na upepo mkali unaozidi Km 40 kwa saa na mawimbi makubwa katika bahari ya Hindi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Tma, Dk.Agnes Kijazi amesema vipindi vya mvua kubwa vinatarajiwa katika Mikoa ya Lindi, Mtwara, Morogoro (Kusini) na Ruvuma.
Dk.Kijazi alisema pia viwango vya joto , mawio na machweo ya jua kwa baadhi ya miji hapa nchini vitabadilika.
“Kutakuwa na hali ya mawingu, mvua na ngurumo katika baadhi ya maeneo na vipindi vifupi vya jua,”alisema Dk Agnes.
                                 
Alisema upepo wa Pwani unatarajiwa kuvuma kwa kasi ya km 40 kwa saa, kutoka Kaskazini-Mashariki kwa Pwani ya  Kaskazini na kutoka Kaskazinikwa Pwani ya Kusini.

TAHARUKI KUSOMBWA KWA KIVUKO DAR



 TAHARUKI imetanda katika maeneo ya Kivuko cha Feri, jijini Dar es Salaam baada ya kudaiwa kivuko cha MV Magogoni kukwama najini na kupoteza uelekeo kutokana na upepo mkali uliokuwa ukivuma jana asubuhi katika Bahari ya Hindi.

FICHUA ilifika maeneo hayo na kukuta baadhi ya wananchi wakielezea tukio hilo ambao walidai kivuko hicho kilipoteza mwelekeo na kusababisha taharuki kwa wananchi wanaotumia usafiri huo.

“ Kuna kivuko leo kilikuwa kimepakia abiria kikasombwa na upepo na kupelekwa umbali mrefu hadi walipopata msaada wa kuvutwa baada ya masaa matatu kuanzia saa moja hadi saatatu asubuhi,” alisema mmoja wa shuhuda aliyejitambulisha kwa jina la Asia Rajab.

Alisema kivuko hicho kilikwama kwa muda wa masaa matatu  hivyo kuleta usumbufu mkubwa kwa wasafiri wanaotumia usafiri huo.

Alisema hali hiyo imewafanya abiria kuogopa kukitumia kivuko hicho kwa hofu ya kuzama majini.
 
Hata hivyo Ofisa Habari wa TEMESA Theresia Mwami alikiri kupata taarifa hizo na kudai kuwa  wanazifanyia kazi na watatoa taarifa itakapokuwa tayari.

Wakati huohuo, Mamlaka ya Hali ya Hewa (Tma), jana imetoa tahadhari wananchi wa Ukanda wa Pwani kwakuwa kutakuwa na upepo mkali unaozidi Km 40 kwa saa na mawimbi makubwa katika bahari ya Hindi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Tma, Dk.Agnes Kijazi amesema vipindi vya mvua kubwa vinatarajiwa katika Mikoa ya Lindi, Mtwara, Morogoro (Kusini) na Ruvuma.

Dk.Kijazi alisema pia viwango vya joto , mawio na machweo ya jua kwa baadhi ya miji hapa nchini vitabadilika.

“Kutakuwa na hali ya mawingu, mvua na ngurumo katika baadhi ya maeneo na vipindi vifupi vya jua,”alisema Dk Agnes.
                                 
Alisema upepo wa Pwani unatarajiwa kuvuma kwa kasi ya km 40 kwa saa, kutoka Kaskazini-Mashariki kwa Pwani ya  Kaskazini na kutoka Kaskazinikwa Pwani ya Kusini.

mwisho

Jumatatu, 4 Januari 2016

NYUMBA ZILIZOWEKEWA X ZAFIKIA 5522



ZOEZI la uwekaji wa alama ya X katika nyumba zilizojengwa  mabondeni jana limeendelea huku nyumba  zaidi ya 3000 zilizojengwa katika bonde la mto Msimbazi ziliwekewa X.
Imeelezwa kuwa tangu kuanza kwa zoezi hilo la uwekaji wa alama hiyo katika  nyumba zilizojengwa mabondeni nyumba zaidi ya 5000  zimewekewa  X  na kwamba kutokana na idadi hiyo inaonyesha kuwa nyumba nyingi zitaathiriwa na bomoa bomoa hiyo.
Kutokana  na vurugu zilizofanyika juzi wakati wa kuanza kwa zoezi hilo la kuweka X katika nyumba hizo za mabondeni, Jeshi la Polisi lililazimika kuimarisha ulinzi ili kuwawezesha wafanyakazi wa Baraza la Taifa la Mazingira (NEMC) kuendelea na zoezi hilo la uwekaji wa alama.
Wakati wa zoezi hilo polisi pamoja na wafanyakazi wa NEMC walilazimika kutembea kwa miguu kutoka Jangwani kuelekea Buguruni Alhamza kwenda na kurudi kutokana na kuwa maeneo hayo hakuna barabara za kupia magari kwa sababu ya ubovu wa miundombinu.
Polisi hao walionekana kupita kila kona huku wakiwa na mabomu ya machozi pamoja na bunduki hali ambayo ilisababisha wananchi kuanza kuzungumza maneno ya kejeli kuwa Chama Cha Mapinduzi ‘(CCM) ni ile ile’ na ‘acha waisome namba CCM mbele kwa mbele’.
Wakati zoezi hilo linaendelea wapo baadhi ya askari walikuwa wakizunguka maeneo ya Round about ya Kigogo ili kuhakikisha kwamba wananchi  hawafanyi vurugu zozote kama kuchoma matairi na kufunga barabara.
Akizungumza baada ya kumaliza zoezi hilo kwa jana Ofisa Mazingira Mwandamizi kutoka NEMC Arnold Kusiraga alisema kuwa zoezi hilo la jana wameweka nyumba zaidi ya 3000 ambapo tangu waanze zimefikia takribani 5500.
“Inavyoonekana nyumba zitakazovunjwa zitakuwa nyingi tofauti na makadirio ya kwanza kwani kwa sasa tumefanya kazi kama robo tu lakini nyumba ni nyingi na maeneo yaliyobaki  bado mengi,”alisema.
Aidha alitaja maeneo ambayo yaliwekewa alama jana kuwa ni Jangwani, Kigogo mbuyuni, Kigogo Sambusa, Mapera, Dampo na Buguruni Alhamza.
Hata hivyo alisema zoezi la kubomoa nyumba linaendelea leo katika maeneo ya Bonde la Mkwajuni hadi Daraja la Sarender ambapo Machine za kubomolewa zimeongezwa kutokana tatu hadi kufikia nane.
Alisema zoezi la kuweka X  linaendelea leo katika maeneo ya Buguruni Kwamnyamani hadi Segerea.
Alisema maeneo mengine yatakayoathiriwa na bomobomoa hiyo ni wale waliojenga kandokando ya mito ambapo aliitaja baadhi ya mito hiyo kuwa ni Mto Msimbazi, Mzinga, Kizinga, Mto Ng’ombe, Tegeta, Mbezi, Mpiji, Mineva na Nyakasangwe

Jumanne, 1 Desemba 2015

BUGURUNI WANUSURIKA MAFURIKO



WAKAZI wa Buguruni  Kwamnyamani wamenusurika kuzama tena kutokana na maji kuingia kwenye makazi yao na kusababisha usumbufu mkubwa baada ya mtaro wa kupitisha maji ambao haujakamilika kujengwa kuziba.
Awali Machi 16, mwaka huu Mtaro huo ulisababisha wakazi hao kuishi katika mazingira magumu baada ya nyumba zaidi ya 300 kujaa maji, hivyo, kumfanya Rais Jakaya Kikwete kufika eneo hilo na kutaka baadhi ya nyumba zivunjwe na ujenzi wa mtaro huo uanze mara moja.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakazi hao walisema wamekuwa wakiishi kwa hofu kwani ujenzi wa mtaro huo umekuwa wakusuasua na kusababisha maji kuingia katika makazi yao pindi mvua zinaponyesha.
Mmoja wa wakazi hao, Abdallah Mtigile alisema mvua zilizonyesha juzi jioni zilisababisha maji kuingia katika makazi yao na kusabisha hofu kubwa na uhalibifu wa mali zao.
“Tunahitaji msaada wa haraka kutokana na mvua ambazo zimeanza kunyesha kwani mtaro huu haupeleki maji kabisa mvua kidogo tu unaziba,” alisema Mtigile.
Alisema hali hiyo imewafanya kutokwenda kazini kwa kuhofia familia zao kupoteza maisha kwa mafuriko kutokana na mvua zilizoanza kunyesha.
“Tunahitaji Rais Magufuli aje aone kupuuzwa kwa agizo la Rais Kikwete, hakuna anayetusikiliza kilio chetu ...tuko hatarini kwa kuwa mamlaka ya hali ya hewa imesema kutakuwepo na mvua kubwa msimu huu,” alisema Mtigile.
Naye Faudhia Ally alisema kuwa maji ya mvua yaliingia ndani huku yakiwa yamechanganyika na maji ya vyooni jambo ambalo linaweza kupelekea magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu kuendelea kuenea eneo hilo.
“Maji yaliyochanyika na uchafu wa vyooni yalifika mpaka mlangoni na kutufanya tushindwe kutoka nje kwa kuhofu magonjwa ya mlipuko… huenda kipindupindu kikaongezeka kutokana na mvua hizi,” alisema Faudhia.
Akizungumza ofisini kwake Mwenyekiti wa serikali ya Mtaa wa Mnyamani, Abdallah Mng’ae alisema amefanya juhudi mbalimbali kutatua tatizo hilo ikiwa ni pamoja na kupiga simu kwa viongozi wa manispaa.
“baada ya maji kuingia kwenye makazi ya watu nilipiga simu kwa uongozi wa manispaa wakasema hawana nafasi na kumtuma dereva wa mashine(Excavator) iliyokuwepo kwenye eneo hilo akafika na kuzibua,” alisema Mng’ae.
Alisema Katibu mkuu alifika eneo hilo hivi karibuni na kuwataka uongozi kumaliza ujenzi wa mtaro huo haraka lakini mpaka sasa bado unasuasua huku mkandarasi akidai kutolipwa fedha za ujenzi. 
Alisema ujenzi wa mtaro huo umekuwa ukijengwa kwa kitumia nondo za hali ya chini hivyo kusababisha kubomoka kabla ya kumalizika.
“Kama mnavyoona karavati walizotumia ni ndogo ambazo ni rahisi kuziba na haziwezi kupitisha maji yanapokuja kwa kasi hivyo kurudi katika makazi ya watu,” alisema.
Fichua ilishuhudia watu wakihamisha samani zao za ndani na kuyahama makazi yao.