ZOEZI la
uwekaji wa alama ya X katika nyumba zilizojengwa mabondeni jana limeendelea huku nyumba zaidi ya 3000 zilizojengwa katika bonde la mto
Msimbazi ziliwekewa X.
Imeelezwa
kuwa tangu kuanza kwa zoezi hilo la uwekaji wa alama hiyo katika nyumba zilizojengwa mabondeni nyumba zaidi ya
5000 zimewekewa X na
kwamba kutokana na idadi hiyo inaonyesha kuwa nyumba nyingi zitaathiriwa na
bomoa bomoa hiyo.
Kutokana na vurugu zilizofanyika juzi wakati wa kuanza
kwa zoezi hilo la kuweka X katika nyumba hizo za mabondeni, Jeshi la Polisi
lililazimika kuimarisha ulinzi ili kuwawezesha wafanyakazi wa Baraza la Taifa
la Mazingira (NEMC) kuendelea na zoezi hilo la uwekaji wa alama.
Wakati wa
zoezi hilo polisi pamoja na wafanyakazi wa NEMC walilazimika kutembea kwa miguu
kutoka Jangwani kuelekea Buguruni Alhamza kwenda na kurudi kutokana na kuwa
maeneo hayo hakuna barabara za kupia magari kwa sababu ya ubovu wa miundombinu.
Polisi hao
walionekana kupita kila kona huku wakiwa na mabomu ya machozi pamoja na bunduki
hali ambayo ilisababisha wananchi kuanza kuzungumza maneno ya kejeli kuwa Chama
Cha Mapinduzi ‘(CCM) ni ile ile’ na ‘acha waisome namba CCM mbele kwa mbele’.
Wakati zoezi
hilo linaendelea wapo baadhi ya askari walikuwa wakizunguka maeneo ya Round
about ya Kigogo ili kuhakikisha kwamba wananchi
hawafanyi vurugu zozote kama kuchoma matairi na kufunga barabara.
Akizungumza
baada ya kumaliza zoezi hilo kwa jana Ofisa Mazingira Mwandamizi kutoka NEMC
Arnold Kusiraga alisema kuwa zoezi hilo la jana wameweka nyumba zaidi ya 3000
ambapo tangu waanze zimefikia takribani 5500.
“Inavyoonekana
nyumba zitakazovunjwa zitakuwa nyingi tofauti na makadirio ya kwanza kwani kwa
sasa tumefanya kazi kama robo tu lakini nyumba ni nyingi na maeneo
yaliyobaki bado mengi,”alisema.
Aidha
alitaja maeneo ambayo yaliwekewa alama jana kuwa ni Jangwani, Kigogo mbuyuni,
Kigogo Sambusa, Mapera, Dampo na Buguruni Alhamza.
Hata hivyo
alisema zoezi la kubomoa nyumba linaendelea leo katika maeneo ya Bonde la
Mkwajuni hadi Daraja la Sarender ambapo Machine za kubomolewa zimeongezwa
kutokana tatu hadi kufikia nane.
Alisema zoezi
la kuweka X linaendelea leo katika maeneo
ya Buguruni Kwamnyamani hadi Segerea.
Alisema maeneo mengine yatakayoathiriwa na bomobomoa
hiyo ni wale waliojenga kandokando ya mito ambapo aliitaja baadhi ya mito hiyo
kuwa ni Mto Msimbazi, Mzinga, Kizinga, Mto Ng’ombe, Tegeta, Mbezi, Mpiji,
Mineva na Nyakasangwe
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni