WANANCHI wa Vijiji vya Koma na
Kwale, Wilayani Mkuranga mkoani Pwani, wanakabiliwa na changamoto ya
ukosefu wa vituo vya afya, hali inayosababisha kupoteza maisha na wanawake
kujifungilia kwenye boti wakati wakifuata huduma hiyo Wilayani.
Wananchi hao walitoa malalamiko yao
mbele ya Mbunge wa Jimbo la Mkuranga, Abdallah Ulega, juzi alipofanya
ziara ya siku moja ya kutembelea visiwa hivyo
kuwashukuru wananchi kwa kumchangua kuwa mwakilishi wao pamoja na
kukagua miradi ya maendeleo.
Mmoja wa wanakijiji hao, Maimuna
Nyakonda, alisema kuwa wanawake wamekuwa
wakipata madhara wakati wakisubiri usafiri wa boti kuwavusha na kuwapeleka
Wilayani Mkuranga kwa matibabu lakini kwa bahati mbaya wamekuwa wakizalia
njiani na wengine kuzalishwa na wakunga kutokana na hali ya hewa.
"Ukosefu wa zahanati katika
Vijiji hivi ambavyo viko kisiwani, umesababisha sisi wanawake kudhalilika sana,
tunajifungulia njiani huku mabaharia wakishuhudia pia wakati mwingine wenzetu
wanapoteza maisha, hili jambo linatusononesha sana, " alisema Maimuna.
Naye Halima Said, mkazi wa kijiji
cha Koma, alisema hali hiyo imesababisha wanawake wa visiwa hivyo kuendelea
kutegemea huduma za wakunga ambao hawana ujuzi na kusababisha madhara kwa
wanaojufungua.
"Huku tunatumia njia mbili tu
kuhamia Wilayani wakati mimba inapofikia miezi nane au kama huna ndugu huko ubaki
hapa, kama Mungu akisaidia kukawa na hali ya hewa nzuri bahari
haijachafuka, unaweza kufika Wilayani salama,” alisema.
Alisema kama ikishindikana wanalazimika
kwenda kwa mkunga ambaye hata hivyo hawana ujuzi wa kumsafisha mama
aliyejifungua vizuri.
Akizungumza tatizo hilo, Ulega
alisema, tayari ameanza kujenga Zahanati katika kijiji cha Koma ambayo
inatarajia kukamilika mwaka huu na katika kijiji cha Kwale ameagiza uongozi wa
kijiji na halmashauri kuanzisha ujenzi ili aweze kuendeleza.
"Natambua shida mnazopata mama
zangu, naahidi mwaka huu hautaisha bila zahanati hii kukamilika lakini pia
naandaa utaratibu wa kujenga nyumba ya mganga, kununua thamani zote za
ndani ili mganga aje tu na nguo, awape huduma wananchi wangu wa Koma,
"alisema Ulega.
Alifafanua kuwa, katika kipindi
chake cha miaka mitano ya uongozi anatarajia kujenga zahanati na vituo
vya afya 30 ili wananchi na wapate huduma ya afya iliyo bora.
MWISHO
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni