Alhamisi, 5 Januari 2017

WALIOUAWA KWA UJAMBAZI WALIPORA MIL.25 TAZARA


JESHI la polisi nchini limesema limebaini kuwa majambazi waliouawa katika tukio la unyanganyi katika jengo la kibiashara la White House Tower lililopo Mikocheni, jijini Dar es Salaam,walihusika pia katika wizi wa  milioni 25  eneo la  Tazara katika makutano ya barabara ya Mandela na Nyerere.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamishna Simoni Sirro alisema baada ya kufanya tukio hilo la wizi katika eneo la Tazara, majambazi hao waliokuwa wanne, walipanga kwenda kufanya tukio lingine katika jengo la White House Tower lililopo Mikocheni. 
“Tukio hilo lilitokea jana(juzi),kwenye muda wa  saa 5:20, eneo la Mikocheni kwenye jengo la kibiashara la White Star Tower, tulipata taarifa kuna hao  majambazi ambao waliofanya tukio kwenye barabara ya Nyerere na kuchukua milioni 25,naamini walinogewa na hizo fedha wakaenda tena kufanya ujambazi.
“Baada ya kupata taarifa hiyo mapema,vijana wetu wakaenda kujipanga na walipoingia,askari wakapiga risasi ili majambazi wajisalimishe lakini nao walijibu, ndipo majibizano yalipoanza na  kuwauwa watatu na kukamata bastola moja aina ya SIG SAUER yenye namba P 229 ikiwa na risasi nne ndani ya magazine,”alisema Kamishna Sirro.
Alisema mmoja wa majambazi hao alifanikiwa kutoroka kwa kutumia usafiri wa pikipiki na jeshi hilo linaendelea kumtafuta.
Kamishna Sirro alisema wataendelea kupambana na suala la unyanganyi wa kutumia silaha katika jiji la Dar es Salaam.
Katika tukio lingine,Kamishna Sirro alisema wanamshikilia mkazi wa Tundwi Songani,kata ya Pemba Mnazi,Wilaya ya Kigamboni, Anwaz Ally kwa kukuta na bastola moja aina ya BARRETA ikiwa na risasi 23.
Alisema silaha hiyo ilipatikana baada ya kupekuliwa maungoni na kumkuta nayo ikiwa imefutwa namba huku akiwa hana kibali halali cha umiliki wa silaha hiyo.
“Mtuhumiwa huyo alipekuliwa katika chumba chake anachoishi ambapo alikutwa na risasi 23 za silaha ya BARRETA aliyokuwa ameificha ndani ya soksi.
“Mahojiano yanaendelea ili kubaini matumizi ya silaha hiyo, kwani kuna taarifa za kutumika kwa silaha hiyo kwenye matukio ya uhalifu katika maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam,”alisema.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni