Jumanne, 1 Desemba 2015

WAANDISHI WAITAKA MAHAKAMA KUWATENGEA ENEO LAO



WAANDISHI wa habari za mahakama nchini wameitaka mahakama kuandaa mazingira rafiki na sehemu bora zitakazowawezesha kufanya kazi zao kwa ufanisi.

Akisoma mapendekezo yaliyotolewa katika mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari za mahakamani yaliyomalizika juzi, mmoja wa waandishi hao, Kulwa Mzee alisema wamekuwa wakipata shida kupata sehemu ya kufanyia kazi zao hivyo kuitaka mahakama kuandaa eneo hilo.

Alisema ili kuboresha kuanzishwe mtandao wa waandishi na mahakama utakaosaidia upatikanaji wa vitu muhimu kama takwimu, hukumu na usajili.

“Tunaziomba Mahakama na Baraza la Habari Nchini(MCT) kuanzisha mafunzo endelevu ya waandishi wa habari za mahakama ambayo yatashirikisha pia wahariri ili kuepuka makosa kutokana na kutojua lugha za kimahakama,” alisema Kulwa.
Alisema katika mapendekezo yao wamewataka Majaji na Mahakimu kutoa nakala za hukumu pamoja na muhtasari kwa waandishi.
“Tunapendekeza Mahakama na MCT kushawishi uanzishwaji wa madawati ya habari za mahakamani katika vyumba vya habari ili kuwasaidia waandishi,” alisema Kulwa.
Kwa upande wake Jaji Kiongozi, Shaban Lila alisema mafunzo hayo ni muhimu katika kujenga mahusiano mazuri kati ya vyombo vya habari na mahakama.
Alisema mhimili wa Mahakama uliwahi kupewa tuzo ya kufuli lililofungwa kuonyesha kuwa walikuwa wagumu kutoa habari zao.
“Tunahitajiana, wote tunafanya kazi kwa ajili ya jamii hivyo tushirikiane kwa kutoa habari zilizosahihi, fasaha na kwa wakati,”alisema Lila.
Alisema Mahakama imekuwa ikilalamikia uandishi wenye mapungufu huku waandishi wakilalamika ugumu wa kupata habari.
“Waandishi wamekuwa wakitumia maneno ya kuhukumu katika uandishi wao kabla kesi haijatolewa hukumu na kusababisha usumbufu kwa jamii walioaminishwa tofauti na hukumu iliyotolewa,” alisema Lila.
Jaji Lila alisema si kwamba mahakama wanakwepa kuambiwa kasoro zao bali ziwakilishwe kwa lugha za staha bila kuwashambulia majaji na mahakimu.
“Hakuna Jaji anayeweza kuamua anavyotaka yeye, anaamua kutokana na sheria na ushahidi, kama kuna tatizo ni upungufu wa sheria husika na si Jaji,” alisema Jaji Lila.
Mwisho


    

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni