WAKAZI wa Kurasini
Shimo la Udongo wamejikuta wakikosa makazi baada ya nyumba 45 walizokuwa
wakiishi kubomolewa ili kupisha upanuzi wa bandari na ujenzi wa maegesho ya
malori.
Ubomoaji huo
ulifanyika jana, saa moja asubuhi hali iliyosababisha wananchi wa eneo hilo
kujikuta wakitawaliwa na vilio, simanzi kutokana na kuharibiwa kwa mali zao
zilikuwemo ndani ya nyumba hizo.
Wakati kazi
hiyo ikiendelea polisi walikuwa wameimarisha ulinzi katika eneo hilo,
wakishirikiana na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), ambao walikuwa na jukumu
la kuzuia kutokea kwa tatizo la umeme kwa nyumba zilizokuwa na nishati hiyo.
Bomoabomoa
hiyo iliwanufaisha vibaka waliokuwa wakivamia na kupora vitu wakati kazi ya
ubomoaji ilipokuwa ikiendelea huku vijana wengine walinufaika na ajira ya uokoaji
kwa kulinda mali zao.
Akizungumza
na FICHUA Diwani aliyemaliza muda wake, Wilfred Kimati alisema, ubomoaji
huo umefanyika kinyume cha sheria kwakuwa wananchi bado walikuwa wakidai malipo
yao.
Alisema eneo
hilo lilifanyiwa tathimini na mthamini kutoka Wizara ya Ardhi Nyumba na Makazi
ambapo wananchi wa eneo hilo walikuwa 161 na walitakiwa kulipwa fidia ya Sh. Bilioni
16.
Kimati
alisema eneo hilo limechukuliwa na mwekezaji kampuni ya Easy Netwotk Solution
ambao walikubali kulipa fidia stahili na eneo hilo litumiwe kwa maegesho ya
magari makubwa.
“Tumebaini
Manispaa ya Temeke ina vitabu viwili vya tathmini ambapo malipo yaliyofanywa yakionyesha
kuwepo makato makubwa kwenye fidia hali iliyosababisha baadhi ya wenye nyumba
64 kufungua mashauri mahakamani kugomea fidia hiyo wakidai walipwe iliyokuwa
imepangwa na wizara,”alisema Kimati.
Kimati
alisema eneo hilo lina nyumba 165 ambapo nyumba 45 ndiyo zimebomolewa zikiwemo
zilizokuwa kwenye zuio la Mahakama jambo ambalo ni ukiukwaji wa sheria.
Kwa upande
wake, mwananchi James Mwakalobo alilalamikia nyumba yake kubomolewa wakati
ikiwa na zuio la mahakama.
Naye,
Mwenyekiti wa mtaa huo, Rajabu Nkumilwa alisema, manispaa hiyo imekiuka kwakuwa
wananchi wake walikuwa na madai ya msingi.
Alisema
wananchi wanalia na upunjwaji wa fidia kwakuwa wengine wamelipwa kiwango cha
chini Sh. Milioni 27 hadi Mil.188 wakati nyumba hizo zilikuwa na hatimiliki na
thamani kubwa.
“Wananchi
walikubali uhakiki wa malipo ya fidia ya Wizara ya Ardhi Nyumba na Makazi
lakini cha ajabu manispaa ya Temeke nao wameingilia kati na kupunja fidia za
wananchi hawa,”alisema Nkumilwa.
Akijibu hoja
hizo Mkurugenzi wa Temeke, Photidas Kagimbo alisema ubumoaji wa eneo hilo
ulikuwa sahihi kwakuwa notisi ilianzia Juni 10 mwaka huu na ilikuwa ya siku 60
na hadi jana wanafanya ubomoaji ilikuwa ni siku 150.
Alisema
wananchi wenyewe walisaini mkataba wa malipo na wengi wao wamepokea malipo hayo
kilichobaki ni kulibadili eneo hilo kuwa la kisasa kwa ajili ya matumizi
kusudiwa.
“ Wananchi
wamedhamiria kuendelea kuishi katika eneo hilo huku wakijua kuwa ni
kunyume…lakini taratibu zimefuatwa na ubomoaji utaendelea ili miradi mingine
iendelee na kuongeza pato la taifa,”alisema Kagimbo.
Naye, Kaimu
Mthamini wa manispaa hiyo, Victor Ndonne alisema mradi huo ulibuniwa na
manispaa tangu mwaka 2006 na tangu wakati huo kumekuwa na hatua mbalimbali za
utwaji maeneo kwa ajili ya shughuli hiyo.
Alisema manispaa
ilimwandikia Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi , Nyumba na Maendeleo ya Makazi ili
itolewe idhini ya kufanya mapitio ya mradi huo.
Ndonne
alisema katibu mkuu alitoa idhini ya mapitio ya mradi huo ambapo manispaa kwa
kushirikiana na mthamini Mkuu wa Serikali walitengua uhalali wa kitabu cha
kwanza na kukubaliana kwa pamoja kutumika kwa kitabu cha pili.
“Mapitio
yalifanyika baada ya mwekezaji kulalamika gharama ya mradi huku kuna miradi
mingine imefanyika kipindi kama hicho na gharama zake zilikuwa chini,”alisema
Ndonne.
Waandishi wa
Mtanzania walishuhudia tingatinga T 502 CZP, T 202 CFN, T 159 BED na T 205 DCS
zikiwa katika eneo hilo zikiendelea na ubomoaji huku baadhi ya wananchi wakiwa
wanalinda mali zao nje wakiwa wamekosa makazi.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni