KATIBU Mkuu wa Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Dk. Vincent Mashinji ni mmoja wa Viongozi wa
Umoja wa Vyama vya Kidemokrasia Duniani (IDU) walioalikwa kukutana na Rais wa
Ghana, Nana Akufo-Addo nchini humo, Jumatano, Juni 21, mwaka huu,
Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano Tumaini
Makene imesema mwaliko huo ni sehemu ya mkutano wa umoja huo utakaofanyika
mjini Accra, Ghana.
Alisema mbali ya kukutana na Rais
Nana Akufo-Addo, Dk. Mashinji atakutana na Rais Mstaafu wa Ghana John Agyekum
Kufuor kwenye mazungumzo yatakayofanyika Juni 20, mwaka huu, baada ya ujumbe huo wa IDU kutembelea Bunge la
Ghana.
“Viongozi hao mbali ya
kubadilishana uzoefu wa mazingira tofauti ya kisiasa, watatumia mkutano huo
kujadili masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na namna ambavyo nchi zao zinaweza
kusimamia misingi ya kidemokrasia kwa ajili ya maendeleo na ukuaji wa kiuchumi,
kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na jinsi ya kunufaika na
ongezeko kubwa la vijana,” alisema Makene.
Alisema mkutano huo wa IDU
ulioanza Juni 19, mwaka huu, unawakutanisha viongozi kutoka nchi mbalimbali
wakiwamo viongozi kutoka Umoja wa Vyama vya Kidemokrasia Afrika (DUA), miongoni
mwao akiwa ni Kiongozi wa Chama cha Forum for Democratic Change (FDC), ambaye
pia ni Mwenyekiti wa DUA Dk. Kizza Besigye kutoka Uganda, Katibu Mkuu wa DUA
Charles Owiredu na Mwenyekiti wa Heshima wa DUA, Peter Mac Manu.
Katibu Mkuu Dk. Mashinji
aliyeondoka Juni 18, kwa ziara hiyo ya kikazi atarejea nchini Juni 22, mwaka
huu.
mwishoDk
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni