Jumanne, 20 Juni 2017

MEYA JACOB AZIDI KUSOTA MAHABUSU

MEYA wa Manispaa ya Ubungo Boniface Jacob(Chadema) ameendelea kusota mahabusu baada ya kukamatwa na Jeshi la polisi jana.
Akizungumza na MTANZANIA Ofisa habari wa Chadema Tumaini Makene alisema taarifa walizonazo ni kwamba anashikiliwa na jeshi hilo kwa amri ya Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Kisare Makori.
Makene alisema mpaka sasa hawajui kosa analotuhumiwa Jacob japokuwa wameambiwa atakaa mahabusu kwa saa 48.
“Ni vizuri umwulize Mkuu wa Wilaya ya Ubungo kuhusu kosa alilotenda Meya kwani hata sisi hatujui kinachoendelea,” alisema Makene.
Alisema viongozi wengine wa Chadema waliofika kituo cha polisi wilaya ya Ubungo walifukuzwa huku Katibu wa Chadema Wilaya hiyo, Justine Mollel, naye akikamatwa baada ya kwenda kumtembelea Jacob.
 Akizungumza na kituo cha runinga cha Azam, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Kisare Makori alisema ameamua kumkamata Jacob kutokana na kukiuka taratibu za kazi kwa kuwaleta wanachama wa Chadema wa kanda ya Pwani na kuwatembeza katika miradi ya maendeleo ya halmashauri.

Makori alisema kwa mujibu wa sheria na taratibu, mwenye mamlaka ya kukagua miradi ya maendeleo ni wajumbe wa kamati ya Maendeleo wa Halmashauri chini uenyekiti wa Meya ama Mwenyekiti wa Halmashauri.
“Hivyo kitendo cha Meya kutembelea miradi ya maendeleo bila madiwani wa kamati husika ni kuvunja sheria,na dawa yake ni kukaa ndani na kufunguliwa mashtaka,” alisema Makori.
Alisema ameagiza pia kukamatwa na kutiwa ndani kwa viongozi wengine waliokuwa katika msafara huo aliwamo Waziri Mkuu mstaafu na Mwenyekiti wa Chadema kanda ya Pwani Frederick Sumaye kujibu ni kwanini walikwenda kutembelea miradi ya maendeleo bila idhini ya mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ubungo.

“Kitendo cha Meya kutumia ukumbi na majengo ya halmashauri kukutana na viongozi wa Chadema ni kinyume na kanuni na sheria za utumishi wa umma,hivyo nimeagiza Meya huyo kukaa ndani kwa masaa 48 kabla ya kufunguliwa mashtaka,huku Sumaye na viongozi wengine wasakwe na kuwekwa ndani.

mwisho


Dk. Mashinji huyoo Ghana

KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Dk. Vincent Mashinji ni mmoja wa Viongozi wa Umoja wa Vyama vya Kidemokrasia Duniani (IDU) walioalikwa kukutana na Rais wa Ghana, Nana Akufo-Addo nchini humo, Jumatano, Juni 21, mwaka huu,
Taarifa iliyotolewa na  Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano Tumaini Makene imesema mwaliko huo ni sehemu ya mkutano wa umoja huo utakaofanyika mjini Accra, Ghana.
Alisema mbali ya kukutana na Rais Nana Akufo-Addo, Dk. Mashinji atakutana na Rais Mstaafu wa Ghana John Agyekum Kufuor kwenye mazungumzo yatakayofanyika Juni 20, mwaka huu, baada ya ujumbe huo wa IDU kutembelea Bunge la Ghana.
“Viongozi hao mbali ya kubadilishana uzoefu wa mazingira tofauti ya kisiasa, watatumia mkutano huo kujadili masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na namna ambavyo nchi zao zinaweza kusimamia misingi ya kidemokrasia kwa ajili ya maendeleo na ukuaji wa kiuchumi, kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na jinsi ya kunufaika na ongezeko kubwa la vijana,” alisema Makene.
Alisema mkutano huo wa IDU ulioanza Juni 19, mwaka huu, unawakutanisha viongozi kutoka nchi mbalimbali wakiwamo viongozi kutoka Umoja wa Vyama vya Kidemokrasia Afrika (DUA), miongoni mwao akiwa ni Kiongozi wa Chama cha Forum for Democratic Change (FDC), ambaye pia ni Mwenyekiti wa DUA Dk. Kizza Besigye kutoka Uganda, Katibu Mkuu wa DUA Charles Owiredu na Mwenyekiti wa Heshima wa DUA, Peter Mac Manu.
Katibu Mkuu Dk. Mashinji aliyeondoka Juni 18, kwa ziara hiyo ya kikazi atarejea nchini Juni 22, mwaka huu.

mwishoDk

serikali yaufyata kwa walemavu


WAZIRI wa Mambo ya ndani na Mbunge wa jimbo la Iramba Magharibi Mkoani Singida, Mwigulu Nchemba leo bungeni amefunguka na kuomba radhi dhidi ya vitendo vya jeshi la polisi kutumia nguvu kubwa kupambana na watu wenye ulemavu.
Mwigulu Nchemba amekiri kuwa jeshi la polisi lilitumia nguvu kubwa mno kwa watu hao na kusema serikali wamepokea jambo hilo na kuahidi kulifanyia kazi ili siku nyingine lisijirudie.
"Kwanza naomba niombe radhi kwa jambo hili na naomba salamu zangu ziwafikie watu wenye ulemavu, ni kweli kwamba kwa kuzingatia hali yao jeshi la polisi lilitumia nguvu kubwa, ila sisi kama serikali tumeshawasiliana na TAMISEMI na kuzungumza nao juu ya mambo yao, lakini pia tumepokea jambo hili na tunalifanyia kazi ili siku nyingine jambo hili lisijirudie" alisema Mwigulu Nchemba
Mnamo tarehe 16, Juni, 2017 jijini Dar es Salaam jeshi la polisi lilitumia nguvu kubwa ikiwepo kuwapiga na kuwadhalilisha watu wenye ulemavu ambao walikuwa wamejikusanya katika barabara ya Sokoine, Posta Jijini Dar es salaam ili kwenda kumuona Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, kuwasilisha malalamiko dhidi ya askari wa usalama wa barabarani kuwakamata na kuwazuia kuingia katika jiji. Lakini pia walikuwa wakipigania haki yao ya kuwa na maeneo ya kuegesha vifaa vyao katikati ya jiji.
CHAMA cha watu wenye ulemavu mkoa wa Dar es Salaam(Chawata),wamelaani kitendo cha wao kunyanyaswa na kupigwa na Jeshi la Polisi walipokuwa wakienda kwa mkurugenzi wa manispaa ya Ilala kupeleka kero zao.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Makamu mwenyekiti wa chama hicho, Hamadi Komboza alisema katika tukio hilo la  Juni 16, Mwaka huu, Mtaa wa Sokoine jijini Dar es Salaam walipigwa na kupandishwa kwenye gari kama gunia.
 “Tulikuwa tunaelekea kwa Mkurugenzi wa Ilala tulipofika njiani askari walituvamia wakarusha mabomu ya machozi na kutupiga huku wakiturusha kwenye gari lao (Difenda) kama gunia,” alisema Komboza.
Alisema walipofikishwa kituo cha polisi waliwekwa mahabusu kwa muda wa saa nane sehemu ambayo ni chafu bila kujali hali zao kwa kuwa wengine hutumia mikono kutembea.
Aliongeza walipokuwa mahabusu walipigwa marungu huku wakiombwa rushwa ya Sh. 10,000 kwa kila bajaji.
“Waliokataa mpaka sasa bajaji zao zinaendelea kushikiriwa na jeshi hilo kituo cha kati na waliolipa waliruhusiwa kutoka,” Komboza.
Mmoja wa waathirika hao GFatuma Abdallah alisema alidhalilishwa kwa kukamatwa na askari wa kiume huku nguo zake zikichanika na kuacha maungo yake wazi.
Akizungumza huku aliwa analia Fatuma alisema alipofikishwa kituo cha kati aliambiwa akaandikishwe kwa askari mwanamke wakati tayari alikuwa amedhalilishwa.
“Nilipokuwa napakizwa ndani ya gari nguo zangu zilichanika na kuacha maungo yangu wazi mbele ya wanaume,” alisema Fatuma.
Wakati huohuo Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imelaani tukio hilo walilofanyiwa walemavu hao.
Taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa tume hiyo Bahame Nyanduga ilisema THBUB imefuatilia tukio hilo kwa kuzungumza na viongozi wa walemavu na mamlaka husika, hususani Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Dar es Salaam na kuelezwa kuwa mnamo Juni 16,Mwaka huu watu wenye ulemavu wapatao 200 wakiwa na vyombo vya moto, vijulikanavyo kama “bajaji”, waliziba barabara ya Sokoine kwa madai ya kutaka Mkurugenzi asikilize madai yao yahusuyo wenzao kukamatwa kwa kuendesha vyombo vyao bila kufuata taratibu za sheria.

“Taarifa za vyombo vya habari na mitandao ya kijamii zilionyesha askari wa Jeshi la Polisi wakiwapiga watu hao wenye ulemavu pamoja na kwamba watu wenye ulemavu walikiuka taratibu za sheria ni wazi kwamba wakati wa kuzuia uvunjifu huo wa sheria, kulikuwa na vitendo vya ukatili na udhalilishaji dhidi ya watu hao wenye ulemavu wakati wakikamatwa na kuingizwa kwenye magari,” alisema Nyanduga.
Alisema hakuna mtu anayepaswa kuvunjiwa haki zake wakati wa kutekeleza sheria.
“Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) Ibara ya 13 (6) (e) ni marufuku kwa mtu kuteswa, kuadhibiwa kinyama au kupewa adhabu zinazomtweza au kumdhalilisha.
Haki hizi pia zimeainishwa ndani ya mikataba mbalimbali ya kimataifa na kikanda ambayo Tanzania imeridhia,” alisema.
Alisema Tume inapenda kulikumbusha Jeshi la Polisi kwamba kukimbilia kuwapiga raia kila wanapoonekana kukinzana na sheria ni matumizi mabaya ya madaraka yao.
“Ni wajibu wa polisi kulinda usalama wa raia bila kuwadhalilisha, kuwatesa na kuwapiga. Matumizi ya nguvu kupita kiasi wakati wa kutekeleza sheria ni uvunjifu wa sheria,” alisema Nyanduga.
Alisema pamoja na uvunjifu wa sheria uliotendwa na watu wenye ulemavu kitendo cha kuwapiga bila kuwapa muda wa kutawanyika, au kutoa hoja za malalamiko yao kupitia kwa wawakilishi wao ni kitendo cha kuwadhalilisha.
“Tume inatoa wito kwa Jeshi la Polisi kuzingatia kanuni, sheria, haki za binadamu na misingi ya utawala bora katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku,” alisema.
Alisema ni vema kwa jeshi hilo kuwapatia mafunzo ya mara kwa mara askari polisi na maafisa wake kuhusu haki za binadamu na misingi ya utawala bora wakati wa kuratibu  na kushughulikia masuala ya maandamano na mikusanyiko ya raia.
“Polisi wahakikishe kuwa maafisa na askari wake hawatumii nguvu kupita kiasi wawapo katika operesheni zinazohusu raia waliokusanyika kwa amani, na hususan watu wenye ulemavu, ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza.
“Tume inatoa wito kwa raia kwa ujumla, wakiwemo watu wenye ulemavu, kwamba hamna mwananchi au mtu yeyote aliye juu ya sheria, na kwamba njia bora ya kutatua kero au matatizo yanayowakuta wananchi wakidai haki zao ni kwa kufuata taratibu za sheria,” alisema Nyanduga.
Alisema anawaomba viongozi wa watu wenye ulemavu wafuate taratibu hizo kufikisha hoja zao kwenye vyombo na mamlaka husika na siyo vinginevyo.
mwisho