WAKAZI wa Wilaya za Kibaha mkoani Pwani Ubungo na Ulala mkoani
Dar es Salaam wameondokana na adha ya upatikanaji wa maji baada ya Mamlaka ya
Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) kuwasha Mtambo mpya wa Ruvu juu juzi
jioni.
Taarifa iliyotolewa na DAWASA imedai kuwa wamewasha mtambo huo baada
ya kazi ya kuunganisha umeme wa kutosha kukamilika Aprili 15, mwaka huu.
DAWASA imedai kuwa kazi ya kuwasha pampu kubwa mpya katika
Mtambo wa Ruvu Juu sasa imekamilika rasmi na sasa mtambo huo utaanza
kuzalisha lita milioni 196 kwa siku.
Taarifa hiyo imedai kuwa kazi mbalimbali zilizofanyika ni pamoja
na ujenzi wa kituo kipya cha kusukuma maji na ufungaji wa pampu mpya, maeneo
mapya ya kusafisha maji, mitambo ya kuchuja maji, maeneo ya kuchuja matope na
tenki kubwa la kuhifadhi maji safi.
“Kituo kipya cha kusukuma maji safi na salama kilijengwa
sambamba na mabomba makuu ya kusafirishia maji hayo yenye jumla ya urefu
wa kilomita 70 kutoka Mlandizi hadi Dar es salaam,” ilidai taarifa hiyo.
Taarifa hiyo pia ilidai kuwa tenki jipya lenye uwezo wa kuhifadhi
lita milioni 10 limejengwa eneo la Kibamba lenye muinuko na kutoka hapo maji
yatashuka kwa nguvu ya mtiririko hadi katika matenki ya Kimara.
“Kazi iliyokuwa imebaki ni kuongeza nguvu ya umeme ili pampu
hizo mpya ziweze kufanya kazi ambayo imekamilika, ukaguzi umefanyika na pampu
moja baada ya nyingine ziliwashwa ili kuhakiksha mfumo mzima sasa unafanya
kazi.
“Hadi kufika juzi jioni Aprili17, maji yalikuwa yanaingia
katika matenki yote kwa kupitia mabomba mapya bila matatizo,” ilisema taarifa
hiyo.
Taarifa hiyo iliongeza kuwa mtambo huo wa maji wa Ruvu Juu sasa
unapokea umeme wa kutosha kutoka katika transfoma kubwa iliyopo kituo kidogo
cha umeme Chalinze (Sub-station) yenye uwezo wa 45/55 MVA ambapo inawezesha
pampu zote mpya zilizofungwa kuwashwa kwa wakati mmoja.
“Mikataba ya jumla ya dola za Marekani 99 ya upanuzi wa mtambo
na ujenzi wa mabomba mapya kutoka Ruvu Juu mpaka Kimara, ujenzi wa tanki kubwa
lenye ujazo wa lita million 10, ofisi kwa ajili ya shighuli za uendeshaji wa
huduma na nyumba za watumishi wa mtambo ilisainiwa mwaka 2014.
Fedha hizo ilikuwa ni mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya
Exim ya India,” ilidai taarifa hiyo.
Kazi inayopewa msukumo mkubwa kwa sasa ni ujenzi wa
miundombinu ya usambazaji maji yaliyoongezeka ili wananchi wengi zaidi waweze
kunufaika na jitihada na uwekezaji uliofanywa na serikali yao.
Maeneo yanayonufaika ni pamoja na miji ya Kibaha, Mlandizi na
baadhi ya Vitongoji vyake karika mkoa wa pwani na maeneo yote yaliyopo jorani
na barabara ya Morogori yaani Kiluvya, Kibamba, Mbezi, Kimara, Ubungo,Malamba
mawili, Msigani, Msakuzi, Makabe, Kibangu, External, Makuburi, Tabata, Segerea,
Buguruni na Vingunguti.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni