SERIKALI
imetoa eneo la hifadhi la Pori la Vikindu lenye
ukubwa wa hekari 50, kwaajili ya ujenzi wa miundombinu ya huduma za
jamii za Kijiji cha Kipala Mpakani, kata ya Mwandege wilaya ya Mkuranga Mkoani
Pwani.
Awali eneo
hilo lilikuwa likimilikiwa na serikali chini ya wizara ya Maliasili na Utalii na
kuwa ni moja ya maeneo ambayo kwa vipindi tofauti yalitumiwa na wahalifu kama
sehemu ya maficho yao kabla ya kudhibitiwa na jeshi la polisi siku chache
zilizopita.
Akizungumza
katika hafla fupi ya kuwakabidhi pori hilo, Waziri wa Maliasili na Utalii Profesa
Jumanne Maghembe alisema serikali imeguswa
na matatizo yanayowakabili wakazi wa eneo hilo zaidi elfu ya elfu kumi kukosa
huduma muhimu za kijamii.
Alisema
anashangaa jamii ya watu wanaohifadhi pori hilo kukosa zahanati, shule, soko na
huduma nyingine za kijamii huku pori hilo likigeuka maficho ya wahalifu.
“Haiwezekani
wanafunzi wanaoishi katika kijiji hiki kutembea kilomita saba kufuata shule
vikindu huku wajawazito na wagonjwa kufuata huduma Mbagala,” alisema Maghembe.
Alisema
baada ya kuona umuhimu wa huduma hizo ameamua kutoa eneo hilo litumuike kujenga
miundombinu ya huduma za kijamii.
“Nawapa hili
eneo lenye hekari 50 kwa ajili ya kujenga huduma hizo na kesho watakuja
wataalamu kupima na kuainisha mipaka hivyo kuanzia sasa nalitoa kwenu,” alisema
Pro. Maghembe.
Alisema
atamwomba Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya makazi, Williamu Lukuvi kutoa
hati miliki ya eneo hilo kwa kijiji hicho.
“Baada ya
miezi mitatu tutatangaza katika gazeti la serikali kuwa pori la Vikindu ni mali
ya wananchi wa eneo hilo,” alisema.
Awali akitoa
taarifa Mbunge wa Mkuranga Abdallah Ulega alisema wanafunzi wanaoishi kijijini
hapo hutembea kilomita 7 kufuata shule iliyopo Kisenvule jambo linalosababisha wengi
kushindwa kumaliza masomo kwa utoro.
“Huduma
nyingi za jamii katika eneo hili zinapata katika kata ya Mbagala mkoa wa Dar es
Salaam hivyo tunahitaji eneo hili kwa ajili ya ujenzi wa zahanati, Shule ya
msingi na sekondari, kituo cha polisi, kituo cha mabasi na huduma nyingine za
jamii,” alisema Ulega.
Mmoja wa
wakazi wa eneo hilo, Amina Seif alisema eneo hilo lilikuwa hatari kwa waharifu
kujificha hivyo watashirikiana na serikali kujenga miundombinu hiyo kwa haraka.
mwisho
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni