Jumanne, 21 Novemba 2017

'kuweni wazalendo'

NAIBU Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Alias Kwandikwa amewataka wataalamu wa ujenzi kuwa wazalendo kwa kuokoa gharama za ujenzi wa majengo mbalimbali ili kulipunguzia mzigo taifa.
Akizungumza katika ziara yake aliyoifanya juzi katika mradi wa ujenzi wa nyumba za Wakazi wa Magomeni Kota jijini Dar es Salaam, Kwandikwa alisema uzalendo unahitajika hasa katika kipindi hiki taifa likiwa katika mageuzi makubwa kiuchumi.
Alisema wataalamu wanatakiwa kuwa wazalendo wakati wakisimamia miradi mbalimbali ya ujenzi ili kuokoa fedha zitakazokwenda katika miradi mingine.
“Wakati tunaangalia matumizi ya miradi ya serikali tujiulize kwenye familia zetu tunafanya hivi?,” alisema Kwandikwa.
Alisema wataalamu wa ujenzi waende kujifunza namna ya kupunguza gharama za ujenzi kwa  Wakala wa Ujenzi Tanzania(TBA) ambao katika miradi yao wamepunguza kwa kiwango kikubwa.
“Endeleeni kuokoa fedha kadri mnavyoweza baadaye mtatuambia kiasi mlichookoa ili zisaidie katika miradi mingine ya kitaifa,” alisema Kwandikwa.
Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa TBA Elius Mwakalinga alisema wataendelea kufanya utafiti wa kushusha gharama za ujenzi ili kuongeza ushindani wa kibiashara.
Alisema mradi wa ujenzi wa nyumba za Magomeni Kota utagharimu Sh Bilioni 20 mpaka kukamilika.
“Uzalendo ndio unaotufikisha hapa kwani vijana tulionao wanatanguliza maslahi ya Taifa mbele,” alisema Mwakalinga.
mwisho    


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni