WAKAZI
wa kijiji cha Kibamba, kata ya Mipeko wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani
wanalazimika kutembea umbali wa kilomita 6 kufuata huduma za afya katika kijiji
cha Mwanambaya.
Akizungumza
katika harambee ya kuchangia ujenzi wa Zahanati, Mtendaji wa kijiji hicho, Ally
Madenge alisema kijiji hicho hakina huduma za afya jambo linalosababisha
wajawazito kujifungua njiani wakielekea kutafuta huduma hiyo.
“Hali
ya huduma za afya kijijini hapa ni mbaya tunalazimika kuzifuata katika kijiji
cha Mwanambaya na Mkuranga… huku tukiwa na wazee na watoto jambo ambalo ni
hatari,” alisema Madenge.
Alisema
kwa kuliona hilo wamelazimika kualika wadau mbalimbali kufanya harambee
itakayosaidia ujenzi wa zahanati kijijini hapo.
Akiongoza
harambee hiyo, Mbunge wa Mkuranga Abdallah Ulega alisema jumla ya shilingi
milioni 98 zinahitajika katika ujenzi wa Zahanati hiyo.
“Niwahakikishie
wote watakaochangia hapa kuwa hatutamvumilia yeyote atakayefanya ubadhilifu wa
fedha ama vitu vitakavyochangwa hapa,” alisema Ulega.
Ulega
alimtaka Diwani wa kata ya Mipeko kusimamia kila hatua ya ujenzi huo kwa
uaminifu na uadilifu mkubwa.
“Niwaombe
vijana wa kijijini hapa mjitolee katika ujenzi huu…hatuwezi kutafuta fedha za
ujenzi na za kulipa vibarua hivyo ili kupunguza gharama hata mimi nitakuja
kushiriki katika kambi ya ujenzi ili tuondokane na hili,” alisema Ulega.
mwisho