Ijumaa, 22 Julai 2016

MIL.463 kukarabati Stand ya Ubungo



HALMASHAURI ya Jiji la Dar es Salaam imepanga kutumia shilingi milioni 463 katika kukifanyia ukarabati kituo cha mabasi yaendayo mikoani cha Ubungo.
Akizungumza na FICHUA, Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita alisema jiji limepitisha mpango wa manunuzi ambao utaruhusu kuanza kwa ukarabati huo.
Alisema ukarabati huo utahusisha ujenzi wa mifumo ya maegesho, vyoo, milango ya kuingilia na taa.
“Jana (Juzi)tumepitisha mpango wa manunuzi ambao tuna mamlaka ya kuanza kazi, na inawezekana kesho(leo) mkaona zabuni zikitangazwa katika gazeti la serikali ambazo zitajumuisha ujenzi wa maegesho, ” alisema Mwita.
Alisema sambamba na hilo wanatarajia kuanza kwa ujenzi wa vituo vitatu vya mabasi yaendayo mikoani na nje ya nchi katika maeneo tofauti.
“Ujenzi huo utakaofanyika kwa ushirikiano wa serikali na sekta binafsi katika maeneo ya Mbezi Luisi kwa mabasi ya mikoa ya kati na magharibi, Boko Basihaya kwa mikoa ya kaskazini na Kongowe kwa mikoa ya kusini.
Mwita alisema kupanda kwa viingilio vya wasindikizaji katika stand ya ubungo kutoka shilingi 200 hadi 300 kunatokana na kupanda kwa gharama za maisha.
“Bei hizi zilikuwapo tangu mwaka 1998 ni tofauti na sasa, na Faida za kuongezwa kwa shilingi mia matunda yake yataonekana baadaye kwa kupata huduma zilizo bora,” alisema Mwita.
Aidha alisema wako katika mikakati ya kuweka kulipanga upya jiji la Dar es Salaam ambapo tayari wameanza kufanya uchambuzi.
“Kwa sasa wanaendelea kufanya tathmini kwa kutumia picha za ndege hivyo kufikia Septemba, Mwaka huu tunaweza kutoa ‘masterplan’,” alisema Mwita.
                                              
mwisho

  
   

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni