Jumatano, 27 Julai 2016

KINONDONI YATUMBUA SABA



BARAZA la Madiwani la Manispaa ya Kinondoni limewachukulia hatua za kinidhamu watumishi wake saba kwa kuwashusha vyeo na wengine kufukuzwa kazini baada ya makosa waliyokuwa wakituhumiwa kuthibitika.
Miongoni mwa watumishi waliochukuliwa hatua ni Mhandisi Mkuu wa Manispaa Hassan Mkuya ambaye ameshushwa cheo na sasa anakuwa mhandisi wa kawaida pamoja na mwenzake Ismail Mafita aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Barabara wa Manispaa.
Meya wa Manispaa hiyo, Boniface Jacob (Chadema) alisema hayo jana wakati alipokuwa akisoma taarifa ya Baraza la Madiwani ambalo ndilo lilipendekeza kuchukuliwa kwa hatua hizo.
“Desemba mwaka jana aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda alitoa tuhuma dhidi ya watumishi wa manispaa hasa idara ya uhandisi, baadae Mkurugenzi naye alichukua hatua ya kuwasimamisha kazi watumishi 18 waliotuhumiwa na kuwafungulia mashauri ya kinidhamu.
“Kati ya hao 18, tisa walikuwa wa idara ya uhandisi, nane idara ya afya na mmoja idara ya fedha. Mhandisi Mkuu alikuwa akituhumiwa kwa makosa sita likiwamo la kutokufanya usanifu uliozingatia weledi hali iliyopelekea gharama za miradi kuzidi na kushindwa kutembelea eneo la miradi na wakandarasi kusababisha hasara za barabara ya Biafra, Journalism phase 2 na ile ya Maandazi,” alisema.
Alisema tuhuma nyingine ni kutotoa cheti cha ukamilishaji kazi, hatujui miradi kama imeshajengwa , kushindwa kusimamia miradi kwa kiwango cha kuridhisha, mfereji wa basihaya kuwekwa  karavati zisizokuwa na kiwango na kuongezeka kwa gharama za miradi ya batabara bila kuzingatia taratibu za kisheria za manunuzi ya umma.
“Kati ya tuhuma hizo zipo ambazo alikutwa na hatia moja kwa moja na nyingine hakukutwa na hatia hivyo ameadhibiwa kulinga na yale aliyokutwa na hatia moja kwa moja kama mfereji wa basihaya na barabara zilizojengwa chini ya kiwango,” alisema.
Alisisitiza adhabu hizo zimetolewa baada ya uchunguzi wa kina kufanyika kwa kushirikiana na vyombo vya dola, uchunguzi ulifanyika kwa kwenda katika maeneo husika ya miradi na watuhumiwa walipewa siku 14 za kujitetea.
Alisema hata hivyo adhabu hiyo waliyopewa haizuii watumishi hao kuchukuliwa hatua zaidi ikiwamo kufikishwa mahakamani.
“Kwa sababu kama hiyo ya fedha za miradi kuzidi, iligundulika kwamba walikubali baadhi ya wakandarasi kufanya kazi huku wakiwa hawajafuata utaratibu wa manunuzi na hadi sasa tunadaiwa Sh bilioni tano, sasa hii ni hasara na baada ya hatua hii tutakutana na hao wakandarasi ili tujiridhishe kama kweli kazi ilifanyika na tutatoa taarifa ya kitakachoamriwa,” alisema.
Pamoja na hayo, daktari mmoja wa Hosptali ya Palestina, Alphonse Chiwambo amepewa onyo kali baada ya kukutwa na kosa la kuomba rushwa ya Sh 30,000 kwa mama aliyekwenda kujifungua.
“Lakini kuna watumishi wanne wa idara ya afya tumewafukuza kazi kwa makosa ya utoro na rushwa na watumishi sita kati ya tisa wa idara ya uhandisi wamerejeshwa kazini baada ya kukutwa hawana hatia,” alisema.
Alisema pamoja na hayo baraza liliridhia kwapandisha vyeo watumishi 372, kubadilisha vyeo watumishi tisa na kuwathibitisha watumishi 206 ambao wamemaliza vipindi vyao vya majaribio na kuonekana kuwa wanafaa kufanya kazi katika utumishi wa umma.


Ijumaa, 22 Julai 2016

MIL.463 kukarabati Stand ya Ubungo



HALMASHAURI ya Jiji la Dar es Salaam imepanga kutumia shilingi milioni 463 katika kukifanyia ukarabati kituo cha mabasi yaendayo mikoani cha Ubungo.
Akizungumza na FICHUA, Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita alisema jiji limepitisha mpango wa manunuzi ambao utaruhusu kuanza kwa ukarabati huo.
Alisema ukarabati huo utahusisha ujenzi wa mifumo ya maegesho, vyoo, milango ya kuingilia na taa.
“Jana (Juzi)tumepitisha mpango wa manunuzi ambao tuna mamlaka ya kuanza kazi, na inawezekana kesho(leo) mkaona zabuni zikitangazwa katika gazeti la serikali ambazo zitajumuisha ujenzi wa maegesho, ” alisema Mwita.
Alisema sambamba na hilo wanatarajia kuanza kwa ujenzi wa vituo vitatu vya mabasi yaendayo mikoani na nje ya nchi katika maeneo tofauti.
“Ujenzi huo utakaofanyika kwa ushirikiano wa serikali na sekta binafsi katika maeneo ya Mbezi Luisi kwa mabasi ya mikoa ya kati na magharibi, Boko Basihaya kwa mikoa ya kaskazini na Kongowe kwa mikoa ya kusini.
Mwita alisema kupanda kwa viingilio vya wasindikizaji katika stand ya ubungo kutoka shilingi 200 hadi 300 kunatokana na kupanda kwa gharama za maisha.
“Bei hizi zilikuwapo tangu mwaka 1998 ni tofauti na sasa, na Faida za kuongezwa kwa shilingi mia matunda yake yataonekana baadaye kwa kupata huduma zilizo bora,” alisema Mwita.
Aidha alisema wako katika mikakati ya kuweka kulipanga upya jiji la Dar es Salaam ambapo tayari wameanza kufanya uchambuzi.
“Kwa sasa wanaendelea kufanya tathmini kwa kutumia picha za ndege hivyo kufikia Septemba, Mwaka huu tunaweza kutoa ‘masterplan’,” alisema Mwita.
                                              
mwisho

  
   

MSONDO FAMILY DAY JUMAPILI



BENDI ya Msondo Ngoma imewataka mashabiki na wapenzi wa muziki wa dansi nchini kujitokeza katika tamasha la siku ya Familia litakalofanyika Julai 31, mwaka huu katika ukumbi wa DDC Kariakoo jijini Dar es Salaam.
Meneja wa bendi hiyo, Said Kibiriti aliliambia DIMBA kuwa lengo ni kuwa na wasaa wa kukutana na mashabiki wao ikiwa ni pamoja na kubadilishana mawazo na kuichangia bendi hiyo ili iweze kufanya vema.
Alisema onesho hilo litawakumbusha mashabiki kuwa bendi ipo na inaendelea kufanyakazi vizuri.
“Katika onesho hilo tunatarajia kutambulisha nyimbo mpya mbili ambazo ni ‘Masimango’ ukiwa ni utunzi wa Edo Sanga na ‘maana ya ndoa iko wapi’ ukiotungwa na mwanamuziki Athumani Kambi,” alisema Kibiriti.
mwisho