Jumapili, 15 Mei 2016

WAJIFUNGULIA KWENYE MABOTI KWA KUKOSA VITUO VYA AFYA



WANANCHI wa Vijiji vya Koma na Kwale,  Wilayani Mkuranga mkoani Pwani, wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa vituo vya afya, hali inayosababisha kupoteza maisha na wanawake kujifungilia kwenye boti wakati wakifuata huduma hiyo Wilayani.

Wananchi hao walitoa malalamiko yao mbele ya Mbunge wa Jimbo la Mkuranga, Abdallah Ulega,  juzi alipofanya ziara ya siku moja ya kutembelea visiwa hivyo  kuwashukuru wananchi kwa kumchangua kuwa mwakilishi wao pamoja na kukagua miradi ya maendeleo.

Mmoja wa wanakijiji hao, Maimuna Nyakonda, alisema  kuwa wanawake wamekuwa wakipata madhara wakati wakisubiri usafiri wa boti kuwavusha na kuwapeleka Wilayani Mkuranga kwa matibabu lakini kwa bahati mbaya wamekuwa wakizalia njiani na wengine kuzalishwa na wakunga kutokana na hali ya hewa.

"Ukosefu wa zahanati katika Vijiji hivi ambavyo viko kisiwani, umesababisha sisi wanawake kudhalilika sana, tunajifungulia njiani huku mabaharia wakishuhudia pia wakati mwingine wenzetu wanapoteza maisha, hili jambo linatusononesha sana, " alisema Maimuna.

Naye Halima Said, mkazi wa kijiji cha Koma, alisema hali hiyo imesababisha wanawake wa visiwa hivyo kuendelea kutegemea huduma za wakunga ambao hawana ujuzi na kusababisha madhara kwa wanaojufungua.

"Huku tunatumia njia mbili tu kuhamia Wilayani wakati mimba inapofikia miezi nane au kama huna ndugu huko ubaki hapa, kama Mungu akisaidia kukawa na hali ya hewa nzuri bahari haijachafuka,  unaweza kufika Wilayani salama,” alisema.
Alisema kama ikishindikana wanalazimika kwenda kwa mkunga ambaye hata hivyo hawana ujuzi wa kumsafisha mama aliyejifungua vizuri.
Akizungumza tatizo hilo, Ulega alisema, tayari ameanza kujenga Zahanati katika kijiji cha Koma ambayo inatarajia kukamilika mwaka huu na katika kijiji cha Kwale ameagiza uongozi wa kijiji na halmashauri kuanzisha ujenzi ili aweze kuendeleza.

"Natambua shida mnazopata mama zangu, naahidi mwaka huu hautaisha bila zahanati hii kukamilika lakini pia naandaa utaratibu wa kujenga nyumba ya mganga,  kununua thamani zote za ndani ili mganga aje tu na nguo, awape huduma wananchi wangu wa Koma, "alisema Ulega. 
Alifafanua kuwa, katika kipindi chake cha miaka mitano ya uongozi anatarajia kujenga zahanati  na vituo vya afya 30 ili wananchi na wapate huduma ya afya iliyo bora.
 MWISHO

Jumapili, 1 Mei 2016

watumishi wa serikali mkoa wa Dar kujengewa nyumba



WAFANYAKAZI wa serikali wa mkoa wa Dar es Salaam wameahidiwa kujengewa nyumba katika viwanja vyao ili kuondokana na kero za kodi za nyumba.
Akizungumza katika maadhimisho ya sikukuu ya wafanyakazi ilivyofanyika kimkoa jijini Dar es Salaam Mkuu wa Mkoa wa huo, Paul Makonda alisema wafanyakazi wamekuwa wakipata taabu nyingi kutokana na mishahara kutokidhi mahitaji ya kodi za nyumba na gharama za maisha.
Alisema mishahara wanayopata haiwezi kutosha kuhimili mazingira ya maisha ya jiji la Dar es Salaam.
“Sisi kama serikali ya mkoa tumekaa na kufikiri kuona namna ya kutafuta watu watakaowajengea nyumba ndani ya miezi sita katika viwanja vyenu nanyi mtalipa taratibu,” alisema Makonda.
Alisema tayari wamenza kutengeneza baadhi ya ramani ambazo wafanyakazi hao watachagua wanazozitaka.
“Mtalipa taratibu kwa kuwa nyinyi ni watumishi wa umma na mimi kama mkuu wa mkoa nitawadhamini,” alisema Makonda.
Aliongeza kuwa katika hatua za uboreshaji wa mazingira ya kufanyia kazi wameanza na walimu ambao ni kundi kubwa kwa kuwawezesha kusafiri bure.
“Lengo langu halikuwa kuishia katika usafiri wa daladala bali utasaidia hata katika mabasi yaendayo kasi japo nilisikitika sana kusikia baadhi ya viongozi wenu kutoa kauli ya kukataa eti kwa sababu wanadai wanamalimbiko na nyongeza ya mishahara.
Leo umenikuta mwenge unaniomba nauli ya kwenda posta kwa daladala mimi nakwambia nina  gari unaanza kutoa sababu za kuwa huna chakula,” alisema Makonda.
Aidha alisema katika kuhakikisha jiji la Dar es Salaam wanatarajia kuachana na matumizi ya mifuko ya plastiki maarufu kama Rambo.
“Niwaombe viwanda wanaotengeneza mifuko hiyo watubadilishie mifuko hii wa ndani ya siku 90,” alisema Makonda.  
Awali akisoma Risala kwa mgeni Rasmi, Mratibu wa maadhimisho hayo, Elias Chizingwa alisema wafanyakazi wa mkoa huo wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwamo mishahara duni isiyokidhi mahitaji hasa katika jiji la Dar es Salaam, wafanyakazi kukatwa kodi mara tatu, baadhi ya waajiri kuchelewesha kupeleka michango katika mifuko ya hifadhi za jamii.
“Changamoto nyingine ni mazingira magumu ya kufundishia walimu, baadhi ya waajiri kutokuvitambua vyama vya wafanyakazi na baadhi ya makampuni ya wawekezaji wa nje kuwanyanyasa wafanyakazi wazalendokwa kuwafanyisha kazi kwa masaa zaidi 18,” alisema  Chizingwa.
mwisho