Jumatano, 3 Februari 2016

TAHARUKI KUSOMBWA KWA KIVUKO DAR



 TAHARUKI imetanda katika maeneo ya Kivuko cha Feri, jijini Dar es Salaam baada ya kudaiwa kivuko cha MV Magogoni kukwama najini na kupoteza uelekeo kutokana na upepo mkali uliokuwa ukivuma jana asubuhi katika Bahari ya Hindi.

FICHUA ilifika maeneo hayo na kukuta baadhi ya wananchi wakielezea tukio hilo ambao walidai kivuko hicho kilipoteza mwelekeo na kusababisha taharuki kwa wananchi wanaotumia usafiri huo.

“ Kuna kivuko leo kilikuwa kimepakia abiria kikasombwa na upepo na kupelekwa umbali mrefu hadi walipopata msaada wa kuvutwa baada ya masaa matatu kuanzia saa moja hadi saatatu asubuhi,” alisema mmoja wa shuhuda aliyejitambulisha kwa jina la Asia Rajab.

Alisema kivuko hicho kilikwama kwa muda wa masaa matatu  hivyo kuleta usumbufu mkubwa kwa wasafiri wanaotumia usafiri huo.

Alisema hali hiyo imewafanya abiria kuogopa kukitumia kivuko hicho kwa hofu ya kuzama majini.
 
Hata hivyo Ofisa Habari wa TEMESA Theresia Mwami alikiri kupata taarifa hizo na kudai kuwa  wanazifanyia kazi na watatoa taarifa itakapokuwa tayari.

Wakati huohuo, Mamlaka ya Hali ya Hewa (Tma), jana imetoa tahadhari wananchi wa Ukanda wa Pwani kwakuwa kutakuwa na upepo mkali unaozidi Km 40 kwa saa na mawimbi makubwa katika bahari ya Hindi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Tma, Dk.Agnes Kijazi amesema vipindi vya mvua kubwa vinatarajiwa katika Mikoa ya Lindi, Mtwara, Morogoro (Kusini) na Ruvuma.

Dk.Kijazi alisema pia viwango vya joto , mawio na machweo ya jua kwa baadhi ya miji hapa nchini vitabadilika.

“Kutakuwa na hali ya mawingu, mvua na ngurumo katika baadhi ya maeneo na vipindi vifupi vya jua,”alisema Dk Agnes.
                                 
Alisema upepo wa Pwani unatarajiwa kuvuma kwa kasi ya km 40 kwa saa, kutoka Kaskazini-Mashariki kwa Pwani ya  Kaskazini na kutoka Kaskazinikwa Pwani ya Kusini.

mwisho

Maoni 1 :