Thursday, May 17, 2018

wakaguzi wa ndani waiangukia serikali


TAASISI ya Wakaguzi wa Ndani (IIA) Tanzania imeiomba serikali kufuata mwongozo wa kimataifa wa weledi wa ukaguzi wa ndani (International Professional Practice Framework) ili kuwawezesha kazi zao kutambulika kimataifa.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa IIA Tanzania, Kafaso Millinga alisema kufuata mwongozo huo kutasaidia Wakaguzi wa Ndani kupata fursa za kufanya kazi hizo katika nchi mbalimbali.
"Tunaiomba serikali kuona umuhimu wa kuufuata mwongozo huu ambao utawasaidia wakaguzi wa ndani kutambulika kimataifa," alisema Millinga.
Alisema katika mwezi wa Mei ambao ni wa kujenga uelewa hivyo wameandaa mihadhara itakayofanyika katika vyuo na taasisi mbalimbali za elimu ili kujenga uelewa wa jamii kuhusu fani hiyo.
"IIA imeandaa mihadhara itakayofanyika katika Chuo kikuu cha Ardhi (ARU), Chuo kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) na Chuo cha Usimamizi wa Fedha(IFM).
"Lengo ni kuuelimisha umma umuhimu wa wakaguzi wa ndani ili kuimarisha maendeleo ya kiuchumi kwa ngazi zote za taifa," alisema Millinga.

alisema pamoja na kutembelea vyuo hivyo pia watakutana na wadau mbalimbali wa maendeleo kuwajengea uelewa juu ya fani hiyo.
Alitoa rai kwa jamii kujifunza na kufuatilia taarifa na ripoti mbalimbali zinazotolewa na Wakaguzi wa ndani ili waweze kupata taarifa sahihi.
"Fani ya ukaguzi wa ndani inahitaji uwajibikaji na uadilifu wa hali ya juu hivyo tunahitaji umma wa watanzania kutupa ushirikiano katika kutekeleza majukumu," alisema Millinga.
Mwisho


Thursday, March 22, 2018

kipindupindu burahati kwa heri


-DAR ES SALAAM
WAKAZI wa Kata ya Mburahati, Manispaa ya Ubungo, jijini Dar es Salaam wataondokana na magonjwa ya mlipuko baada ya kuanza kwa ujenzi wa mradi wa uondoshaji maji taka katika kata hiyo.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi, Mhandisi mradi kutoka Borda ambao ndio wajenzi, Modekai Sanga alisema mradi huo ukikamilika utawanufaisha wakazi 40,000 wa Mburahati na maeneo jirani.
Alisema wakazi hao watapata huduma ya uondoshaji wa majitaka kwa gharama nafuu na hivyo kuondokana na magonjwa yatokanayo na uchafuzi wa mazingira hususani majitaka.
“Katika mradi huu kutapatikana nishati ya gesi ambacho ni lita 7,000 kwa siku, Mboji na maji ya kumwagilia bustani na miti,” alisema Sanga.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Kisare Makori alisema serikali inaendeleza juhudi za ujenzi wa miradi mbalimbali ya kuondosha majitaka kwa kushirikiana na wadau.
Alisema lengo la serikali ni kuwapatia wakazi wa jiji hilo huduma ya uondoshaji majitaka kwa asilimia 30 hadi kufikia mwaka 2020.
“Miradi hiyo ni uboreshaji na upanuzi wa mfumo wa maji taka kwa jiji la Dra es Salaam ikiwa ni pamoja na ujenzi wa mitambo mitatu ya kisasa ya kusafishia maji katika maeneo ya Jangwani (mita za ujazo 200,000),” alisema Makori.
Aliongeza kuwa miradi mingine ni ule wa Kurasini ambao utakuwa na uwezo wa kuondosha majitaka  mita za ujazo 11,000 na wa Mbezi Beach (16,000).
Akizungumzia mradi wa uondoshaji maji Mburahati Makori alisema Ofisi ya Mkoa huo ilisaini makubaliano na shirika lisilo la Kiserikali la Borda la nchini Marekani kujenga mradi huo.
“Mapenda niwapongeze Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam(Dawasa) kwa kushirikiana na Borda kutekeleza mradi huu ambao utawanufaisha wakazi wa Mburahati,” alisema Makori.
mwisho  

Sunday, February 25, 2018

tumieni bidhaa za viwanda vya ndani

na tunu nassor



WATAALAMU wa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji wameshauriwa kutumia bidhaa zinazozalishwa nchini katika kutekeleza miradi ya maji ili nchi kuangalia mikataba wanayoingia ili nchi inufaike na miradi hiyo.
Akizungumza katika ziara aliyoifanya jijini Dar es Salaam, Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Jumaa Aweso alisema wataalamu hao waangalie mikataba wanayoingia ili kuruhusu baadhi ya vifaa vya ujenzi kununuliwa nchini.
Alisema kwa sababu nchi hii kwa sasa ni ya viwanda hivyo ni vyema wanapoingia mikataba kuondoa vipengele vitakavyowafunga katika kununua baadhi ya vifaa.
"Si busara vifaa kama koki na pampu kununuliwa nje ya nchi wakati vinapatikana hapa nchini,” alisema Aweso.
Alisema kwa kufanya hivyo kutasaidia kuongeza mitaji katika viwanda vya ndani, ajira na kuongeza mzunguko wa fedha nchini.
"Pamoja na kuwa na nia njema ya kuwapatia wananchi maji safi na salama lakini pia waliangalie hili kwa manufaa ya nchi,” alisema Aweso.
Aidha aliongeza kuwa bado kuna changamoto ya kuwapo kwa makandarasi wasiokidhi vigezo ambao hutekeleza miradi chini ya kiwango.
“Bado tuna changamoto ya makandarasi wanaopewa miradi 'kiushemeji shemeji' jambo ambalo linasababisha kushindwa kuteteleza kwa kiwango hivyo kama wizara tutawatapisha fedha hizo na kuzirudisha katika miradi," alisema Aweso.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Ufundi kutoka Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam(Dawasa), Modester Mushi alisema wanatarajia kuwaunganishia maji wateja 376,000 katika visima vya Mpera na Kimbiji.
Mwisho

dawasa, dawasco pelekeni maji pembezoni mwa mji


Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Jumaa Aweso ameziagiza DAWASA na DAWASCO kuhakikisha zinafikisha huduma ya maji kwenye maeneo yaliyo pembezoni mwa Jiji la Dar es Salaam, ambapo kuna uhaba mkubwa wa maji pamoja na kuwa na wakazi wengi zaidi na si kujikita katikati ya jiji hilo tu.Naibu Waziri Aweso ametoa agizo hilo akiwa katika ziara ya kikazi katika Wilaya ya Temeke kujionea uhalisia wa utekelezaji wa miradi ya maji, wilaya ambayo imekuwa na malalamiko mengi kuhusiana na huduma hafifu ya majisafi  na salama.Aweso amesema kuwa kuna haja ya DAWASA na DAWASCO kuimarisha huduma ya maji kwenye maeneo ya pembezoni mwa jiji kama Temeke, Kigamboni, Ukonga, Mbagala na Segerea ili kukidhi mahitaji makubwa ya maji kwa wakazi wengi wanaoishi maeneo hayo.''Fanyeni utaratibu wa kukarabati miradi ya zamani kama hatua ya kwanza na ya haraka ya kuwapatia wananchi maji, wakati mkiendelea kutekeleza miradi mipya na mikubwa ambayo utekelezaji wake utachukua muda mrefu. Mmejikita sana katikati ya jiji, ambapo kwa sasa huduma hiyo imeimarika kwa kiasi kikubwa. Umefika wakati wa kuwekeza maeneo ya pembezoni kwa sasa, na wakazi hawa nao wafurahie huduma ya maji ya uhakika'', aliagiza Naibu Waziri Aweso.Aidha, Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji alitoa onyo kwa manispaa zote za Jiji la Dar es Salaam kutowapa kazi wakandarasi wasio na uwezo. Pia, kuchukua hatua stahiki kwa wakandarasi wote wanaosuasua katika utekelezaji wa miradi, huku akiwahakikishia wakandarasi wote kulipwa fedha zao kwa wakati ili wasikwame katika

Tuesday, November 21, 2017

'kuweni wazalendo'

NAIBU Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Alias Kwandikwa amewataka wataalamu wa ujenzi kuwa wazalendo kwa kuokoa gharama za ujenzi wa majengo mbalimbali ili kulipunguzia mzigo taifa.
Akizungumza katika ziara yake aliyoifanya juzi katika mradi wa ujenzi wa nyumba za Wakazi wa Magomeni Kota jijini Dar es Salaam, Kwandikwa alisema uzalendo unahitajika hasa katika kipindi hiki taifa likiwa katika mageuzi makubwa kiuchumi.
Alisema wataalamu wanatakiwa kuwa wazalendo wakati wakisimamia miradi mbalimbali ya ujenzi ili kuokoa fedha zitakazokwenda katika miradi mingine.
“Wakati tunaangalia matumizi ya miradi ya serikali tujiulize kwenye familia zetu tunafanya hivi?,” alisema Kwandikwa.
Alisema wataalamu wa ujenzi waende kujifunza namna ya kupunguza gharama za ujenzi kwa  Wakala wa Ujenzi Tanzania(TBA) ambao katika miradi yao wamepunguza kwa kiwango kikubwa.
“Endeleeni kuokoa fedha kadri mnavyoweza baadaye mtatuambia kiasi mlichookoa ili zisaidie katika miradi mingine ya kitaifa,” alisema Kwandikwa.
Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa TBA Elius Mwakalinga alisema wataendelea kufanya utafiti wa kushusha gharama za ujenzi ili kuongeza ushindani wa kibiashara.
Alisema mradi wa ujenzi wa nyumba za Magomeni Kota utagharimu Sh Bilioni 20 mpaka kukamilika.
“Uzalendo ndio unaotufikisha hapa kwani vijana tulionao wanatanguliza maslahi ya Taifa mbele,” alisema Mwakalinga.
mwisho    


Elimu ya Ufundi changamoto kwa viwanda

TANZANIA inakabiliwa na upungufu wa walimu wa elimu ya ufundi jambo ambalo linasababisha baadhi ya vyuo vya ufundi stadi kuajiri walimu wasiokuwa na sifa zinazohitajika katika fani hiyo.
 Mpaka sasa kuna idadi ndogo ya vyuo vinavyofundisha ualimu wa ufundi stadi jambo linalosababisha kuwapo na walimu wasiokuwa na sifa katika vyuo vya elimu ya Ufundi.
Vyuo vya  mafunzo ya Ufundi stadi ni nguzo pekee ya kulisaidia taifa kuingia katika uchumi wa viwanda mwaka 2020 huku nchi ikitegemea kuingia katika uchumi wa kati.
Hivi karibuni Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi(NACTE) kwa kushirikiana na Kituo cha elimu ya watu wazima Kouvola kutoka nchini Finland waliandaa mkutano wa Kimataifa ili kubadilishana uzoefu kati ya nchi hizi mbili.
Mkutano huo ulibeba ujumbe wa ‘wekeza katika elimu ya ufundi ili Tanzania iweze kuingia katika uchumi wa viwanda’ umehuhudhuliwa na taasisi za elimu ya ufundi, wamiliki wa viwanda, wadau na wataalamu 30, wa sekta hiyo kutoka nchini Finland.
Mkurugenzi wa Maendeleo ya Elimu nchini Finland Dk.Tuija Arola anaelezea nchi hiyo ilivyoweza kuwekeza katika mafunzo ya wakufunzi wa elimu ya ufundi.
Anasema kuna umuhimu wa nchi kuwa na walimu waliobobea katika elimu ya ufundi stadi ili kuweza kutoa wahitimu waliokuwa na sifa za kukidhi soko la ajira.
“Walimu wa mafunzo ya ufundi stadi wanatakiwa kuwa na mafunzo endelevu katika kipindi chote cha ualimu wao ili kwenda na mabadiliko ya kasi ya teknolojia,” anasema Dk. Arola.
Anasema walimu wanatakiwa kutembelea katika maeneo ya viwanda kupata ujuzi mpya unaohitajika katika wakati husika.
Anasema Tanzania inatakiwa kuwekeza katika kuwaandaa wakufunzi wa mafunzo ya ufundistadi ili kufanikisha malengo ya kuwa nchi ya viwanda.
Akitolea mfano katika nchi ya Finland Arola anasema taaluma ya ualimu na ukufunzi nchini humo inathaminika na kuheshimika jambo ambalo linawaongezea nguvu wakufunzi katika kutekeleza majukumu yao.
Anasema kwa kuwa mafunzo ya wanafunzi huhamishiwa katika maeneo ya kazi hivyo wakufunzi wana wajibu wa kuratibu ushirikiano na kampuni zenye kutoa ajira kwa ajili ya kuboresha mazingira ya kazi.
“Mkufunzi ana nafasi kubwa katika kuwezesha juhudi za kujifunza kwa mtu mmoja mmoja ili kufikia malengo yake binafsi,” anasema Dk. Arola.
Anaongeza kuwa kutokana na hali hiyo wakufunzi wa mafunzo ya ufundi wanatakiwa kuwa na elimu ya kiwango cha juu katika fani zao.
Anasema wakufunzi wa elimu ya ufundi wanatakiwa kutumia mbinu mbadala katika kuongeza kiwango chao cha elimu na ujuzi.
Aidha anazitaka mamlaka husika katika kusimamia elimu ya ufundi kuwatengenezea mazingira ya kazi wakufunzi hao ikiwa ni pamoja na kuwapa motisha ili waweze kutimiza majukumu yao kikamilifu.
“Mabadiliko ya utendaji kazi wa walimu unahitaji kujitolea zaidi hivyo watafanikiwa iwapo tu watapata ushiriki na kuungwa mkono na mamlaka ikiwa ni pamoja na kuwawezesha kifedha,” anasema Dk.Arola.
Kwa upande wake Waziri wa Elimu Sayansi, Teknolojia na Ufundi Profesa Joyce Ndalichako anasema serikali inawekeza katika kuwaandaa walimu wa elimu ya ufundi ili kuwa na wataalamu wataoiwezesha nchi katika kuingia katika nchi ya viwanda.
Anasema nchi haiwezi kuingia katika uchumin wa viwanda bila kuwekeza katika raslimali watu watakaofanya kazi katika viwanda hivyo.
“Tujitathmini kuinua ubora wa elimu ya ufundi kwa kuchukua uzoefu kutoka kwa wenzetu kutoka Finland kwa kuwa wenzetu wamefanikiwa katika elimu ya ufundi,” anasema Profesa Ndalichako.
Anasema changamoto iliyopo ni muunganiko wa ubunifu unaofanywa na taasisi za mafunzo ya ufundi na viwanda.
“Changamoto ni namna ya kuunganisha ubunifu unaotolewa na taasisi za mafunzo kuingizwa katika maisha ya kawaida ya watanzania,” anasema Ndalichako.
Profesa Ndalichako anasisitiza juu ya mafunzo ya walimu na wahitimu katika taasisi za juu ili kuendana na mahitaji ya soko la ajira.
“Niwaombe tufanye kazi kwa kushirikiana taasisi za mafunzo na waajiri kuangalia namna ya kupunguza utengano uliopo kwa kuwa kila mmoja anamtegemea mwenzake,” anasema Ndalichako.
Naye Kaimu Katibu Mtendaji wa NACTE, Dk.Adolf Rutayuga anasema Baraza hilo linahakikisha kuwa wahitimu wanaotolewa na vyuo vilivyosajiliwa wanakidhi vigezo vya ajira na mahitaji ya soko.
Anasema kwa kuwa katika mkutano huo walikuwapo pia watoa maamuzi akiwamo waziri Ndalichako hivyo yatafanyiwa kazi na kupata suluhisho mapema.
“Hapa tumekuwa na viongozi wakubwa na watoa maamuzi hivyo yote yaliyozungumziwa katika mkutano huu yatapatiwa ufumbuzi kulingana na mahitaji,” anasema Dk.Rutayuga.
Anasema hii ni hatua moja ya kuelekea katika uchumi wa viwanda kwa kuwa waliokutana hapa ni wadau wakubwa katika sekta hiyo.
“Yamejadiliwa mengi katika mkutano huu hii ni hatua moja mbele kuelekea Tanzania ya Viwanda kwa kuwa tunaunganisha nguvu kwa maana ya Watoa Mafunzo na waajiri ama wenye viwanda,” anasema Dk. Rutayuga

Marufuku kusambaza takwimu za uchumi hila kibali

Na TUNU NASSOR 
DAR ES SALAAM 
OFISI ya Taifa ya Takwimu (NBS ) imewaonya watu wanaotoa takwimu za Uchumi bila kuzingatia sheria ya Takwimu jambo ambalo linasababisha mkanganyiko katika jamii. 
Akizungumza katika maadhimisho ya siku ya Takwimu Afrika, Mkurugenzi Mtendaji wa NBS, Dk Albina Chuwa alisema hairuhusiwi kutoa takwimu hizo bila kuwa na kibali cha NBS. 
Alisema NBS haikatazi mtu binafsi wala kikundi cha watu kukusanya takwimu isipokuwa kinachotakiwa ni kufuata taratibu ikiwa ni pamoja na kupata kibali kutoka katika Ofisi hiyo. 
"Hatumnyimi mtu kibali cha kukusanya kuchakata na kusambaza takwimu isipokuwa kinachotakiwa ni kukusanya kulingana na misingi na sheria namba tisa ya Takwimu, " alisema Dk. Albina. 
Alisema ukusanyaji huo unahitaji weledi wa hali ya juu chini ya kanuni 10 za Takwimu za Dunia. 
" kinachonishangaza takwimu za serikali zinapotolewa mtu anasimama na kusema takwimu hizi si sahihi... Hii inatokea Tanzania pekee, hivyo asitokee mtu kupotosha takwimu za Uchumi " alisema Dk Albina. 
Alisema takwimu za Uchumi ni muhimu kwa utekelezaji wa ajenda ya Afrika ya mwaka 2063.
"Katika ajenda hii kitu kimojawapo ni ukuaji wa uchumi wa bara hilo na haiwezi kufanikiwa bila kuwa na takwimu bora za Uchumi,"  alisema Dk Albina. 
Naye Mkurugenzi wa Uchumi na Sera wa Benki Kuu ya Tanzania(BOT), Johnson Nyella aliwataka wananchi wanaoshiriki katika ukusanyaji wa takwimu kutoa taarifa sahihi wanapojaza dodoso za takwimu